Paul Pogba amekiri kwamba alimsikiliza mama yake wakati anataka kurudi Manchester United kwa usajili uliovunja rekodi ya Dunia wa paundi milioni 100.
Usajili wa Mfaransa huo umekamilika usiku wa Manane kuamkia leo baada ya kuwasili jana AON Training Complex kuchukua vipimo vya Afya.
Kiungo huyo wa zamani wa Juventus, katika mahojiano yake ya kwanza tangu arejee England, amesema miaka minne aliyokaa Seria A ilikuwa kama likizo tu.
Akizungumza kwa mara ya kwanza na MUTV, Chaneli ya Televisheni ya klabu, Paul Pogba ameeleza: "Sina maneno kiukweli, sina maneno. Nimerudi Carrington, ni kama nimerudi nyumbani.
"Inaonekana kama vile nilikwenda likizo na nimerudi tena nyumbani. Nina furaha, namuona kila mtu, watu ni walewale, kiukweli nina hisia kubwa sana".
"Nadhani ni hatma. Kwanza mama yangu aliniambia nitarudi hapa. Nilimwambia, huwezi kujua, tutaona.
"Kwangu mimi ni changamoto kubwa kurejea pale nilipotokea, pale nilipokulia na pale nilipoanzia. Sikumaliza kile nilichoanza hapa, kwahiyo nadhani nitamaliza kila kitu"
0 comments:
Post a Comment