Tuesday, June 2, 2015


Na Shaffih Dauda

UCHAGUZI wa FIFA umefanyika mwishoni mwa juma lililopita mjini Zurich, Uswizi, huku dunia nzima ikishuhudia Sepp Blatter akitetea kiti chake cha urais kwa muhula wa tano mfululizo.

Stori ya uchaguzi mkuu wa FIFA iligonga vichwa vya wanamichezo duniani na ikapata uzito wa juu zaidi siku moja kabla ya kupiga kura ambapo maafisa sita wa ngazi za juu wa Shirikisho hilo walikamatwa na FBI kwa tuhuma za rushwa ya zaidi ya dola za Kimarekani milioni 100.

Kashifa hii nzito ilitikisa dunia na mashinikizo yakaanza kutolewa yakimtaka Rais Blatter ajiuzulu na baadaye aahirishe uchaguzi mkuu kwasababu ya tuhumu hizo.

Msimamo wa Blatter , mwenye uwezo mkubwa wa kuongoza soka ulibaki palepale, uchaguzi ukafanyika mei 29 mwaka huu na yeye kushinda.

Kukaa madarakani kwa muda mrefu, ni sababu inayowafanya watu wengi waamini Blatter hafai, lakini kashifa hii ya rushwa ambayo ni propaganda ya nchi za Magharibi iliwaongezea nguvu watu wasiompenda Blatter akiwemo rais wa Uefa,  Michel Platini.

Kimsingi, hizi kelele za Blatter hafai, ni propaganda za mataifa ya magharibi hususani Marekani. Kwa wale wote wanaompiga vita Blatter, wafanye uchunguzi,  waje hapa watuambie ufisadi upi umefanyika ndani ya FIFA.  Dhahiri hakuna tuhuma za rushwa ndani ya FIFA kama taasisi , ila hizi tuhuma tunazozisikia zimetokea kwenye vyama vingine.

 Wanachama wa FIFA ni vyama vya soka vya nchi na siyo vyama vya mabara kama wengi wanavyodhania, mfano tuhuma za rushwa zinazozungumzwa kuihusisha FIFA zinatokana na chama cha soka cha America ya kaskazini (CONCACAF ).

Concacaf si mwananchama wa FIFA , ndio maana FBI imewakamata kina Jack WARNER pamoja na Jeffrey WEBB kwasababu wao ndio walikuwa viongozi waliohusika kwenye madili hewa yaliyotokana na haki za matangazo ya televisheni pamoja na kuingia mikataba kibao ya kifisadi.

Ukifuatilia kwa undani, mataifa ya magharibi hususani Marekani wanaamini kuwa wao ndio wenye nguvu zaidi duniani ‘Super Power’. Hawafurahii kuona nchi nyingine duniani inawazidi kiuchumi, kibiashara, kiasa n.k

Inapotokea taasisi kama FIFA ambayo si ya kiserikali inakuwa na nguvu kubwa,  wafuasi wengi na wanaongezeka kadri siku zinavyokwenda, Marekani hawafurahii hali hii.

Rais wa FIFA, Sepp Blatter anaonekana ndiye rais mwenye nguvu kuliko rais yeyote duniani, anaweza kumzidi hata rais wa Marekani, Barack Obama.

Blatter ni rais wa dunia wakati Wamarekani wanaamini rais wao ndiye rais wa dunia, lakini kutokana na nguvu ya mpira wa miguu, Blatter anamzidi nguvu Obama.

Kutokana na hali hii, Taifa la Marekani linatafuta namna ya kuidhoofisha FIFA na wana tafuta njia ya kuliweka Shirikisho hilo chini ya himaya yao.

Nikupe mfano wa UN ambayo ni taasisi isiyo ya kiserikali yenye nguvu duniani. Wakati wa utawala wa katibu mkuu, Boutros Boutros-Ghali kutoka Misri (1992-1996), UN ilionekana inakua sana na kuwa na nguvu kupita maelezo.

 Marekani chini ya Rais Bill Clinton (1993-2001) hawakufurahishwa  na nguvu iliyoonekana UN. Walitafuta namna ya kumdhoofisha Boutros ili asiendelee kuwa katibu mkuu katika uchaguzi uliofuata kwasababu alikuwa na mitazamo iliyoikuza taasisi hiyo.

Waliona UN inakuwa na ushawishi na umaarufu kuliko serikali ya Marekani, hivyo wakatafuta kila njia ya kumuangusha Boutros ili taasisi hiyo iwe chini ya himaya yao.

Hii ni sawasawa na sasa ambapo Marekani wanaingia kwenye vita ya kulidhoofisha shirikisho la soka ulimwenguni FIFA  linaloonekana kuwa na nguvu kubwa.  Kutokana na ukubwa wa sasa wa FIFA, inawezekana rais wake, Sepp Blatter akawa na nguvu kuliko hata rais Obama.

Jambo la pili; watu kama Uingereza pamoja na Uefa kwa ujumla ni wabaguzi. Wao wanaamini waanzilishi wa FIFA ni Uefa. Ukiangalia historia ya FIFA iliyozaliwa mjini Paris Ufaransa, iliundwa na mataifa ya bara la ulaya kama vile Ubelgiji, Denmark, Uholanzi, Hispania, Sweden na  Switzerland.

Uefa wao wanadai FIFA ni Shirikisho ambalo chanzo chake ni wao, hivyo sio haki kwa mataifa mengine wanachama wa FIFA kutoka mabara mengine kuwa na nguvu sawa na mataifa ya ulaya.

Ukinukuu kauli ya rais wa Uefa, Michel Platini kwamba; “Ni jambo la aibu kwa nchi kama  Ufaransa kuwa na nguvu sawa na ki-nchi kama Vanuatu”.

Hii ni kauli ya kibaguzi kwasababu katika mchakato wa kupiga kura popote duniani, hakuna kura yenye nguvu kuliko nyingine. Hata wakati Michel Platini anachaguliwa kuwa rais wa Shirikisho la soka Ufaransa, hakukuwepo na kura ambayo inasema matajiri wana nafasi ya ziada ya kupiga kura 10 kuliko maskini.  Inapokuja ishu ya uchaguzi kura ya tajiri na kura ya mtu yeyote mwenye sifa zinafanana.

Kauli ya Platini kwamba nchi kama Ufaransa sio haki kuwa na kura sawasawa na nchi ndogo kama Vanuatu ni ya  kibaguzi moja kwa moja.

Vanuatu ni nchi ndogo ambayo inawakilisha nchi nyingi maskini hususani kutoka bara la Afrika na Asia ambako kuna mataifa mengi masikini, lakini kuna kura nyingi za FIFA.

Uefa wanataka rais wa FIFA atokee kwao, wanataka mtu wao akiingia madarakani wabadilishe katiba kwa mfano kipengele cha timu zinazoshiriki kombe la dunia.

Wakati wa nyuma, nafasi nyingi walipewa Uefa na nafasi chache walitoa barani Afrika na mabara mengine. Blatter ndiye aliyeongeza nchi za Afrika kushiriki kombe la dunia na hayo ni moja ya mafanikio yake katika utawala wake. Amesababisha mataifa kama Togo, Angola, China yapate nafasi ya kushiriki kombe la dunia tofauti na huko nyuma .

Falsafa ya Blatter ya kuendeleza mpira duniani kote  na kusambaza misaada bila upendeleo, imemfanya awe na nguvu zaidi na kuyakera mataifa makubwa hususani ya Uefa pamoja na Marekani. Wanaona kama vile wanakuwa na haki sawa na mataifa madogo kutoka Afrika na mabara mengine.


TAASISI YA FIFA KUHUSISHWA NA RUSHWA


Kashifa ya rushwa wanayohusishwa FIFA ni hila iliyoanzishwa kuharibu uchaguzi wa FIFA.

Kama nilivyoeleza kwa ufupi mwanzoni mwa makala hii ni kwamba; waliotuhumiwa na rushwa ni vyama vya soka vya mabara mengine hasa CONCACAF ambao sio wanachama wa FIFA.

Wanachama wa FIFA ni yale mataifa 209. Zile dili za kupiga dola zaidi ya milioni 100 zilitokana na mikataba ya udhamini mbalimbali pamoja na hela za haki za matangazo ya televisheni ambayo vyama vya mabara ya  Amerika kaskazini na kusini waliingia.

Hiyo kesi inawahusu waliokamatwa kama vile Jeffrey Webb ambaye alikuwa rais wa CONCACAF.  Mtu kama Webb anaishi Miami Marekani na makao makuu ya CONCACAF yapo mjini humo. Kwanini FBI baada ya kufanya uchanguzi wao hawakumkata akiwa Miami na wakasubiri wakati wa uchaguzi wa FIFA?

CONCACAF ndio wenye hatia ya hizo fedha, kwanini wasikamatwe huko huko mpaka wasubiri siku moja kabla ya uchaguzi wa FIFA mjini Zurich?

Lengo la Marekani lilikuwa ni kuhamisha malengo ya uchaguzi na kutengeneza mazingira kuwa FIFA ni chombo cha wahuni na wala rushwa, lakini FIFA kama taasisi haihusiki kwa chochote na ndio maana Blatter hajakamatwa.

Jack WARNER wakati anaingia FIFA alikuwa makamu wa rais wa CONCACAF,  huyu Jeffrey Webb  ni makamu wa rais wa sasa wa CONCACAF.  Kumbuka  hawa wanaingia moja kwa moja kwenye kamati ya utendaji ya FIFA wakiwa makamu wa Rais.

Katiba ya FIFA inasema kwamba marais wa vyama vyote vya mabara kama CAF, UEFA, CONCACAF wanaingia moja kwa moja kama makamu wa rais wa FIFA. Wajumbe wa kamati ya utendaji wanachaguliwa kutoka kwenye vyama hivyo hivyo kutokana na idadi ya nafasi iliyotengwa kutoka kila chama cha bara.

Maana yake ni kwamba wale wajumbe wanaoingia kwenye kamati ya utendaji ya FIFA wanachanguliwa na mabara yenyewe. Makamu wa rais wa FIFA anachaguliwa na nchi wanachama wa vyama vya mabara husika.

Blatter hajakamatwa kwasababu zile fedha hazikupigwa moja kwa moja kutoka makao makuu ya FIFA,  zilizopigwa kwenye vyama na ndio maana wamekamatwa hao viongozi.

Propaganda za mataifa ya magharibi ilikuwa ni kupotosha umma kwamba FIFA kama taasisi imehusika na rushwa  na kumchafua Blatter ili wapiga kura waogope kumchagua, bahati nzuri, wajumbe walibaki kwenye misimamo yao na mwisho wa siku Blatter akashinda na kubaki kuwa rais wa FIFA.


UKIRUDI KWENYE KIPENGELE CHA KUKAA MUDA MREFU MADARAKANI


Toka Blatter alivyoingia madarakani mwaka 1973 akiwa kama kalani tu ‘Development Officer’ alifanya kazi nzuri. Baadaye akateuliwa na rais wa wakati huo wa FIFA, Mbrazil João Havelange kuwa katibu mkuu baada ya kugundua kuwa Blatter amesomea shahada ya biashara na amebobea kwenye mambo ya masoko.

Blatter alikuja na mbinu mbalimbali za kuiingizia fedha  FIFA na moja ya mafanikio yake ya mwanzoni ni kuwezesha kampuni ya Adidas kuwa mdhamini wa FIFA. Pia akawezesha kampuni ya Cocacola kuwa mdhamini wa FIFA.

Zaidi ndiye aliyetengezea timu kabambe ya wataalamu mbalimbali ambao wameliendesha shirikisho kiuweledi na kufungua mianya ya kupata hela zinazosababisha kuwa taasisi yenye nguvu kubwa duniani.

Ukiangalia maendeleo mengi ya mpira yamekuja kipindi cha utawala wake na kauli ya kusema amekaa sana madarakani hivyo atoke  na waje watu wengine wenye mawazo ya kileo sio sahihi.

Ni vitu gani vya kileo ambavyo havijafanyika kwenye utawala wa Blatter? Kupitia teknolojia, ni watu wangapi wameshuhudia fainali za kombe la dunia kupitia kiganjani?

Ni makampuni mangapi ya kibiashara yameingia mikataba na FIFA kwa ajili ya kudhamini michezo mbalimbali? Unaposema  Blatter atolewe kwasababu amekaa sana madarakani, sidhani kama ni kigezo sahihi.

Kwa mfano hapa Tanzania tuchukulie Rais wa TFF, Jamal Malinzi ameingia madarakani, ametengeneza mifumo bora ya soka la vijana, mifumo mizuri ya ligi na vilabu vya Tanzania inayozalisha wachezaji wengi wanaoweza kushindana na mataifa mengine yanayoendelea, lakini amekaa kwa muda mrefu madarakani.

Katika kipindi chake, timu zote za taifa zinashinda na kufuzu kombe la Mataifa ya Afrika na dunia, lakini wanakuja watu wanasema Malinzi atoke kwasababu amekaa madarakani kwa mihula minne, hivyo aje mtu mwingine katika muhula wa tano.

Kigezo cha kumtoa mtu madarakani ni kukaa kwa muda mrefu au kwasababu ameshindwa kufanya kazi? Kama mtu amefanya kazi kwa muda mrefu na imeonekana, kwanini aondolewe?

Katika utawala wa Sepp Blatter vimejengwa viwanja vya kisasa zaidi ya 200. Mataifa madogo kama Haiti, Vietnam, wanacheza mpira kwenye viwanja bora. Unataka mafanikio gani?

Alichotaka kufanyiwa Blatter ni sawa na alichofanyiwa Muammar Gaddafi na mataifa ya magharibi hususani Marekani.

Gaddafi alikaa madarakani kwa muda mrefu, lakini alifanya kazi nzuri, aliboresha miundombinu ya kijamii, wananchi wake walitibiwa bure, walisoma bure, walipewa fedha za kujenga nyumba, alisaidia kwa kiasi kikubwa bajeti ya umoja wa Afrika AU, alitoa michango mingi kwa nchi za Afrika, hata Tanzania aliijengea msikiti mkubwa pale Dodoma.

Kiongozi huyu alifanya mambo makubwa kuliko mtu yeyote Afrika na pengine dunia yote. Nchi yake ni tajiri na alikuwa na uwezo wa kufanya lolote lile analota kwa waanchi wake, lakini mataifa ya magharibi yalimezea mate utajiri wa Libya.

Baadaye wakatafuta namna ya kumdhoofisha Gaddafi,  wakipandikiza chuki na hatimaye akaondolewa madarakani na kuuwawa kabisa.

Hata katika historia ya Iraq , nchi yenye utajiri wa mafuta, Marekani walikuwa wanautaka utajiri huo, walipandikiza chuki miongoni mwa watu, wakapigana na baadaye Rais Saddam Hussein  akauawa na wakafanikisha jambo lao.

Viongozi wazuri wanaondolewa kwasababu tu ya kukaa kwa muda mrefu madarakini, inawezekana baadhi yao wakawa na matatizo kweli, lakini waliowengi ni propaganda za watu wa magharibi hususani wanapotaka jambo lao litimie.

Kwa mifano hiyo, Sepp Blatter sio mtu mbaya, Wamarekani wanatafuta njia ya kumuangusha wakitaka taasisi ya FIFA iwe kwenye himaya yao kama walivyofanya kwa UN, lakini nguvu ya kura imeendelea kumuweka madarani.


Nawatakia siku njema!

0 comments:

 
voyeur porn porn movies sex videos hd porno video