Wednesday, June 10, 2015

Na Oswald Ngonyani
Hatimaye shirikisho lenye dhamana ya mpira wa miguu nchini (TFF) limetoa maamuzi yake kuhusu sintofahamu ya kimkataba baina ya klabu ya Simba dhidi ya mchezaji wake Ramadhani Singano maarufu kwa jina la Messi.


Hayakuwa maamuzi yaliyotegemewa na wengi, yamekuwa ni maamuzi yanayoenda sawia na dhana ya ‘Funika kombe mwanaharamu apite’.TFF hawajawapa mashabiki haja yao ya kumjua mtuhumiwa halali wa sakata hilo, wengi wetu tumejikuta tukibaki na labda.


Pamoja na suala hilo kuhitimishwa na Uongozi wa juu wa TFF chini ya Katibu wake Bw. Celestin Mwesigwa bado kumekuwa na minong’ono ya wazi miongoni mwa wanafamilia ya mchezo wa soka nchini huku wengi wao wakiyaona maamuzi ya shirikisho hilo kama ya kupepesa macho ama kutikisa masikio.


Binafsi nililifuatilia kwa umakini mkubwa sakata hilo tangu lilipoanza kuchipuka wiki kadhaa zilizopita mpaka jana (Jumanne) lilipohusisha wahusika wa pande zote mbili kwa lengo la kufikia maafikiano.


Juu ya maamuzi hayo ya TFF kumeonekana kuwa na utata wa wazi kabisa huku Katibu mkuu huyo akionekana  kushindwa kulifafanua vema sula hilo la kimkataba na  hata kushindwa kutoa majibu stahiki kuhusu tamati ya mikataba miwili iliyokuwa inakinzana ule unaoisha mwaka 2015 na ule wa mwaka 2016.


Wanahabari wengi walitaka kujua tatizo lililokuwa kwenye mkataba lilikuwa ni lipi hasa. Lakini bado kulionekana kuwa na ugumu kwa watoa ufafanuzi akiwemo Mwenyekiti wa Spotanza, Mussa Kisoki ambaye alionekana kuridhia maamuzi ya TFF kirahisi sana na hata kuwashangaza wengi akiwemo Singano mwenyewe.


Ninakumbuka wakati sakata hilo likipangiwa siku ya kutolewa maamuzi Bw. Kisoki alionekana kuzungumza mengi kuhusu haki stahiki za mchezaji husika lakini kauli yake baada ya maamuzi hayo imeonekana kukiuka kile ambacho alikuwa anakisimamia kabla.


Kimsingi wengi tulitegemea makubwa kutoka kwa Kisoki ambaye alikwenda katika kikao hicho kama Mwenyekiti wa chama cha wacheza soka Tanzania (Spotanza) na wengi tulitegemea kuona akimsimamia Ramadhani Singano kinaganaga na hata ikiwezekana  kuhoji maswali magumu kwa Simba lakini pia kwa TFF kwa lengo la kuziondoa sintofahamu zote zilizokuwa zimejitokeza, lakini hakufanya hivyo.


Katika kikao hicho cha jana TFF wamegundua kuwa mikataba yote miwili yaani ule alionao mchezaji lakini pia ule  walionao Simba, ina matatizo na hivyo Katibu huyo wa TFF amewataka wahusika wa pande zote mbili wakubaliane upya.


Maamuzi hayo kwa kiasi  fulani yameonekana kumweka babaikoni hata Singano mwenyewe kwani kilichoamriwa katika kikao hicho kwake kimeshindwa kumpa uhuru wa kujua kama yupo huru au bado ni mchezaji wa Simba.


Kwa wiki kadhaa sasa Simba imekuwa ikisisitiza kuwa ina mkataba na Messi wa miaka mitatu unaoisha mwaka 2016 lakini yeye mwenyewe amekuwa akisisitiza kuwa alikuwa na mkataba wa miaka miwili na klabu hiyo na unaisha Julai mwaka huu 2015.


Utata huo kwa kiasi fulani ulionekana kujenga picha fulani katika vichwa vya wengi huku mtuhumiwa sahihi aliyegushi mkataba akionekana kutafutwa kwa lengo la kuwajibishwa na mamlaka husika za kisheria ili kutoa funzo kwa wengineo wenye unasaba na hulka hizo za kihuni lakini kwa maamuzi haya yaliyotolewa ni wazi kuwa kuna upande ambao haujatendewa haki na TFF.


Kuwaambia wahusika wakae chini na kuzungumza upya suala hilo huku mikataba yao ya awali ikifutwa inaonyesha ni namna gani TFF imeamua kutuzuga watanzania kwa kumficha mharifu.


Kilichokuwa kinalalamikiwa na kila upande ni uhalali wa mkataba. Wakati Singano akiamini kuwa mkataba wake wa miaka miwili ulikuwa sahihi, Simba nao walikuwa wameweka bayana kuwa mkataba wao wa miaka mitatu ulikuwa sahihi pia.


Kwa mantiki hiyo, mkinzano huo wa hoja za kimantiki kutoka kwa kila pande ziliwafanya wadadisi wengi wa masuala ya soka kwenda mbali zaidi na kuamini kuwa kulikuwa na kila dalili ya upande fulani kuhusika katika kugushi mkataba husika, na kilichokuwa kinasubiriwa na wengi ni kuufahamu upande huo uliokuwa umehusika kuupotosha ukweli.


Kwa maamuzi haya ya TFF, ambayo yameonekana kuwa kama ya busara kwa watu wac hache ni wazi kuwa sisi wapenda haki tumewekwa katika mabano na hata kushindwa kujua kipi ni nini, hasa kuhusu mtuhumiwa wa kitendo hicho cha kihuni.


Kuna mambo ambayo yalionekana kutoeleweka na hata kuwafanya waandishi waonekane wakihoji sana hususan kuhusu Suala la kuzingatia mkataba mama jambo ambalo limezidi kuwachanganya hata waandishi lakini katibu huyo alipoulizwa, alionekana kuwa na majibu ya namna ile ile ya kuzidi kuwaweka kwenye mabano waandishi hao.


“Hatujaja hapa kutangaza mshindi ni nani, kwa kifupi ni vizuri waanze upya na kujadili kuhusiana na mkataba mpya,” alisema.


Messi alikuwa na mkataba unaoisha mwaka 2015, wakati Simba wana mkataba unaoisha 2016 jambo lililozua tafrani kati yao.


Licha ya Mwesigwa kukiri kulikuwa na mapungufu pande zote mbili baada ya kikao hicho cha pande zote pamoja na Spotanza, bado alishindwa kuweka wazi kama Messi bado ni mchezaji wa Simba au makubaliano yanamfanya awe huru.


“Siwezi kuweka hadharani masuala yanayohusu mkataba, hiyo ni siri kati ya mchezaji na klabu,”alisisitiza.


Tangu kutolewa kwa maamuzi hayo, wadau wengi wa mchezo wa soka wameonekana kutoridhishwa na kilichoamuriwa huku wengine wakienda mbali zaidi kwa kuilaumu TFF hasa kutokana na kitendo chake cha kuuficha ukweli kuhusu sakata hilo.


Binafsi nilitegemea upande fulani kuwajibishwa kwa kosa la kukiuka sheria na taratibu za kimkataba ili kuwa somo kwa wengine. Lakini kwa maamuzi haya yaliyotolewa ninajilaumu kwa kupoteza muda wangu bure kuisubiri hatma ya sakata hili lililoonekana kuwagusa wengi.


Hii ndiyo soka ya Bongo Bwana…..



(0767 57 32 87)


0 comments:

 
https://www.sexmutant.com/ https://www.sexindrag.com/ porn movies sex videos hd porno video