KOCHA, Piet De Mol raia wa Ubelgiji aliyewahi kuripotiwa
kutua Msimbazi kurithi mikoba ya Goran Kopunovic ingawa haijawa hivyo,
ameendelea kuonyesha nia ya kutua kwenye klabu ya wakata miwa, Mtibwa Sugar,
baada ya viongozi wa timu hiyo kuthibitisha kuwa juzi Jumatatu alitembelea
klabuni hapo.
Licha ya kutofanya mazungumzo yoyote ya
kumpa mkataba, lakini uongozi huo umesema kuwa kocha huyo alifika Manungu,
Turiani kwa ajili ya kuangalia mandhari pamoja na kambi ya wachezaji kwa ujumla
na namna wanavyoishi.
Msemaji wa Mtibwa Sugar, Thobias Kifaru, alithibitisha ujio
wa kocha huyo klabuni hapo ambapo alidai kuwa licha ya kuwatembelea lakini bado
hawajafanya mazungumzo yoyote kuhusu usajili japokuwa nia ya kuzungumza naye
ipo.
“Ni kweli jana (juzi) Jumatatu De Mol alifika hapa klabuni
kwa ajili ya kucheki mandhari pamoja na kambi ya wachezaji wetu kwa ujumla.
“Licha ya kutua hapa, hatuna maana ya kwamba tumeshamsajili,
hapana, tunaomba tu mashabiki wetu wawe na subira, pindi tutakapomalizana naye
tutawajuza kinachoendelea kwani nia tunayo juu yake,” alisema Kifaru.
0 comments:
Post a Comment