Hatimaye sasa Azam FC nayo imeanza kutanua makucha na tayari
imetua kwenye timu maarufu Afrika, TP Mazembe ya DR Congo na kutaka saini za
wachezaji wawili hatari wa timu hiyo.
Taarifa makini zilizopatikana kutoka kwa mmoja wa mabosi wa
ngazi ya juu Azam, zimebainisha mpango huo wa kuwataka wachezaji hao raia wa DR
Congo walio kwenye kikosi cha kwanza cha Mazembe ambao mmojawao anamudu nafasi
ya beki wa kulia na mwingine ni straika.
Chanzo hicho kimefafanua kuwa imekuwa ngumu kuwashawishi
wachezaji hao na sasa wamemua kumtumia mshambuliaji wa timu hiyo, Mtanzania,
Mbwana Samatta ambaye alikubali na ameonyesha kupata mafanikio makubwa katika
kukamilisha zoezi hilo.
Taarifa zinaeleza kwamba awali wachezaji hao ambao mpaka
sasa majina yao bado ni siri, walikuwa wagumu walipoelezwa suala la kuhama
Congo na kuja kukipiga Tanzania lakini baadaye baada ya kushirikishwa Samatta
ambaye ni straika tegemeo wa timu hiyo, sasa mambo yameanza kulainika na
mchakato unakwenda vizuri.
“Kuna wachezaji kwa sasa tunawatafuta kwa ajili ya kuweka
mambo sawa msimu ujao na kuzidi kusonga mbele zaidi ya hapa tulipo sasa, tayari
kuna harakati za kumpata beki mmoja wa kulia na mwingine ni straika, wote raia
wa Congo.
“Wanacheza TP Mazembe, tuliamua kumtumia Samatta kwa kuwa
awali ilikuwa ngumu kuwapata,” alisema bosi mmoja wa Azam.
Alipoulizwa Mtendaji Mkuu wa Azam FC, Saad Kawemba, juu ya
suala hilo alikana na kusema: “Hakuna suala kama hilo.”
SOURCE: CHAMPIONI
0 comments:
Post a Comment