TIMU ya soka ya Tanzania, Taifa Stars imechapwa mabao 2-0 na
Madagascar katika mechi ya pili ya kundi B ya michuano ya Cosafa iliyomalizika
usiku huu.
Hiki ni kipigo cha pili kwa Stars kwani mechi ya ufunguzi
iliyopigwa juzi walichapwa 1-0 na Swaziland.
Kwa matokeo hayo, Madagascar wanaendelea kuwa vinara wa
kundi B kwa kupata pointi zote sita katika mechi mbili za kundi B, wakifuatiwa
na Swaziland walioshinda 1-0 dhidi ya Stars.
Lesotho waliochapwa 2-1 na Madagascar mechi ya kwanza
wanachuana na Swaziland usiku huu majira ya saa 2:30 kwa saa za Tanzania.
Stars wanaendelea kuburuza mkia kundi B, juu yao wapo Lesotho ambao hawana pointi, lakini
wamefunga angalau goli moja na Stars hawajafunga goli lolote katika mechi mbili
walizocheza mpaka sasa.
Kwa matokeo hayo, Stars imetupwa nje ya michuano kwasababu
hata wakishinda magoli 100-0 dhidi ya Lesotho mechi ya mwisho, tayari
Madagascar wamefikisha pointi 6 ambazo Stars hawezi kuzifikia na wana
mchezo mmoja mkononi,
Timu pekee inayoweza kufikisha pointi 6 ni Swaziland ambayo
inacheza leo na Lesotho.
Kama Swaziland watashinda leo, maana yake fainali ya kundi B
itakuwa kati yake na Madagascar ili kupata mshindi mmoja wa kwenda robo
fainali, wakati Stars na Lesotho watakuwa wanachoma ‘mahindi’ nyumbani.
Magascar walishindi 2-1 katika mechi ya kwanza ya kundi B
dhidi ya Lesotho, kwahiyo waliingia katika mechi ya leo dhidi ya Stars wakijua nini cha
kufanya.
Kwanza walikuwa na mpango wa kufunga magoli ya mapema ili
kujiweka mazingira mazuri ya kushinda na kwa bahati nzuri walifanikiwa kufunga
goli dakika ya 13 ambalo liliwaondoa mchezoni Taifa Stars.
Stars walifungwa goli hilo kwa shambulizi la kushitukiza
(Counter-attack) wakipitia upande wa kushoto ambako amecheza Oscar Joshua.
Katika kipigo cha Stars cha 1-0 dhidi ya Swaziland, Oscar
alichemsha mno upande wa kushoto, leo amerudia tena kucheza chini ya kiwango
ingawa hastahili lawama zote kwasababu kuna wachezaji wengine walioshindwa
kutekeleza majukumu yao.
Licha ya makosa kuanzia safu ya kiungo ambapo Mwinyi
Kazimoto, Said Ndemla na Salum Abubakar walishindwa kupunguza kasi ya shambulizi
la kushitukiza la Madascar, Oscar alikuwa amepanda sana, lakini kurudi ikawa
mtihani.
Winga wa Madagascar alikimbia kupiga krosi wakati Oscar
ambaye hana kasi siku zote akishindwa kurudi kwenye eneo lake kwa haraka na
kumpa urahisi mpigaji krosi.
Kwa bahati nzuri Salim Mbombe, Aggrey Morris, na
Mwinyikazimoto walifika eneo lao haraka, lakini nao wakashindwa kuwa na utashi
mzuri.
Badala ya mmoja kumwangalia mpiga krosi na wengine kufanya
maarifa ya kumzuia mshambuliaji, wote wakapeleka akili kwa mpigaji krosi na
mfungaji wa goli akakaa eneo zuri bila usumbufu, alipopata mpira wa krosi
alifanya kazi rahisi kumfunga Deogratius Munishi ‘Dida’.
Mazingira yale yale ya goli la kwanza, Stars walifungwa goli
la pili kwa aina ile ile ya shambulizi la kushitukiza.
Huwezi kumlaumu moja kwa moja Oscar, kwasababu Stars imefanya vibaya safu ya kiungo
hususani kiungo wa Ulinzi alipocheza Sure Boy.
Sijui Nooij aliingia na akili gani, lakini kwa kawaida Sure
Boy hana uwezo wa kucheza nafasi ya kiungo wa ulinzi. Yeye na Kazimoto
walishindwa kuwasaidia mabeki wa kati, Mbonde na Aggrey, hivyo mashambulizi ya
hatari ya kushutukiza ya Madagascar yamefanya kazi nzuri kipindi cha pili.
Kutokana na Stars kukosa kiungo wa ulinzi asilia, ndipo mawazo ya wengi kumtaka Jonas Mkude (Simba) yanaonekana kuwa ya maana.
Kutokana na Stars kukosa kiungo wa ulinzi asilia, ndipo mawazo ya wengi kumtaka Jonas Mkude (Simba) yanaonekana kuwa ya maana.
Kipindi cha pili Nooij alimtoa Mrisho Ngassa na kumuingiza
Simon Msuva, pia akamtoa Said Ndemla na kumuingiza Shomari Kapombe.
Pia alimtoa Juma Luizio na nafasi yake kuchukuliwa na
Ibrahim Hajib Migomba.
Mabadiliko hayo yaliongeza uhai kidogo kwa Stars, lakini bado
hawakuweza kutengeneza mipango mizuri ya kufunga magoli.
Kapombe na Msuva mara kadhaa walijitahidi kulazimisha
kuingia na kupiga mipira ndani, lakini ‘Uchovu’ wa John Bocco aliathiri mipango
hiyo.
Madagascar waliingia kipindi cha pili kwa staili ile ile,
walipanga mashambulizi ya kushitukiza, walikaba kitimu, walijua maeneo muhimu
ya kuwazuia Stars yaani kiungo ili kutoshambuliwa.
Wataalamu wa mpira wa miguu wanasema wachezaji wanaishi
kwenye kivuli cha kocha, wanacheza kuakisi mbinu na ufundi wa kocha wao na ndio
maana timu inapoboronga, kocha ndiye mtu wa kwanza kuwajibika.
Kocha anafukuzwa,
wachezaji wote wanaweza kubaki, lakini kwa Bongo baadhi ya wachezaji pia
wanaweza kupewa adhabu timu inapofanya vibaya ikiwemo kusimamishwa kama
inavyotokea kwa Simba na Yanga.
Wachezaji wa Taifa Stars waliowengi hawako fiti na kwa
bahati mbaya hawajaandaliwa vya kutosha, lakini inafika wakati unaweza kuhoji
uwezo wa kocha Nooij kwa namna timu yake inavyocheza pamoja na uteuzi wake.
Mbinu na ufundi wake
umefeli kwa soka la Tanzania ingawa ni kocha mzuri, hana namna ya kukwepa
lawama.
Timu haina uwezo wa kukaba inapopoteza mpira, mipango ya upigaji wa mipira ya kutenga ni mibovu, wachezaji hawajui wakae wapi na wafanye nini inapotakiwa kufanya maamuzi ya haraka hususani safu ya kiungo na ulinzi.
Timu haina uwezo wa kukaba inapopoteza mpira, mipango ya upigaji wa mipira ya kutenga ni mibovu, wachezaji hawajui wakae wapi na wafanye nini inapotakiwa kufanya maamuzi ya haraka hususani safu ya kiungo na ulinzi.
Mtu kama Erasto Nyoni amekosa kasi kwasababu hajacheza mechi
za mwisho za ligi kuu kutokana na majeruhi, nadhani kocha angeweza kuangalia
wachezaji wengine kama akina Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ (Simba), David
Luhende (Mtibwa), Hassan Kessy (Simba), Juma Abdul (Yanga), Hassan Mwasapili (Mbeya
City).
Hawa ni baadhi ya vijana waliocheza kwa kiwango kikubwa mno
msimu uliomalizika mei 9 mwaka huu, lakini washambuliaji pia ni shida.
Unamuachaje Rashid Mandawa aliyefunga magoli 10 na kumchukua John Bocco ambaye
amefunga magoli matatu tena anasumbuliwa na majeruhi?
Naheshimu mtazamo wa Nooij, lakini ilikuwa nafasi nzuri ya
kujaribu vipaji vipya katika ‘Bonanza’
la Cosafa kwasababu baadaye timu inakabiliwa na michezo migumu zaidi ya kufuzu
CHAN na AFCON.
Kama wachezaji hawa ambao wamezoeleka watacheza hivi hivi
kwenye mechi za kufuzu michuano ya Afrika hapo baadaye, Nooij hatafika popote.
Hata kama atapata wachezaji wengine wanaopendekezwa na wataalamu wa
soka, muda wa maandalizi utatosha? Naamini
hakukuwa na ulazima wa kuwaita baadhi ya wachezaji kama Oscar Joshua, Erasto
Nyoni, John Bocco, Amri Kiemba na wengineo. Ni wachezaji wazuri, lakini kuna
wengine waliochipukia na kufanya kazi zuri.
Mart Nooij anapaswa kupewa muda zaidi wa kuifundisha Taifa
Stars au imefika wakati wa kumuondoa?
Nitumie maoni yako, kosoa mtazamo wangu
Na Baraka Adson Mpenja
Mtangazaji wa Mpira wa Miguu-Azam TV
Tel: 0712461976
0 comments:
Post a Comment