Friday, May 22, 2015


John Bocco (kulia) ameshindwa kuonesha makeke kwenye michuano ya Cosafa


AWALI ya yote nianze kwa kumpongeza nahodha wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars katika michuano ya Cosafa inayoendelea huko Afrika kusini, John Raphael Bocco ‘Adebayor’.
Bocco ameandika makala ndefu na kuiweka kwenye akaunti yake ya facebook na mtandao huu imeichapisha kama ilivyo asubuhi  ya leo, akijaribu kueleza masikitiko yake juu ya soka la Tanzania linalozidi kuporomoka kila sekunde, hususani kuboronga kwa Taifa Stars.
Nimeisoma makala hiyo kwa umakini na kurudia mara nyingi, hatimaye nimeguswa na namna Bocco anavyojua sababu za soka la nchi hii kushuka kila kukicha. Hata Swaziland na Madagascar hatuwawezi kwasasa? Hii ni fedheha.
Mshambuliaji huyo wa Azam fc ni miongoni mwa wahanga wa matokeo mabovu ya Taifa Stars kule Afrika kusini,  hawezi kukwepa lawama kutokana na kiwango kibovu alichoonesha katika safu ya ushambuliaji ya Taifa Stars.
Bocco hayuko fiti hata kwa asilimia 40, amesumbuliwa na majeruhi kwa muda mrefu, hajacheza katika timu yake ya Azam fc, amefunga magoli matatu tu. Hata kocha wake anajua hayuko fiti, lakini Mart Nooij ameona yuko fiti, jiulize mwenyewe utapata jibu.
Wapenda michezo wengi wamemponda Bocco na bila shaka amekuwa akisoma kwenye mitandao ya kijamii jinsi anavyoshambuliwa. Kwa binadamu yeyote ambaye hana moyo wa chuma, lazima aumizwe na matusi, kejeli zinazotolewa na mashabiki kuihusu Taifa Stars.
Ukiyapima maandishi ya Bocco, unagundua kwa haraka kwamba kuna kitu kipo kichwani mwake. Matusi yamemuumiza sana na ili kujaribu kupungumza mzigo uliopo moyoni mwake ameamua kueleza baadhi ya sababu zinazoathiri soka la Tanzania, mathalani;
                      1.       Kutokuwa na program za kuendesha mpira kisasa

                 2 .        Kutokuwa na misingi endelevu ya kuendesha wachezaji wadogo kisasa

                  3.        kutokuwa na ligi kuu bora nchini .

                     4.       Kuwa na uhaba wa wachezaji wanaocheza nje ya nchi ndani ya timu ya TAIFA

                5.       Kutothamini na kuheshimu wachezaji wakitanzania walio ndani ya ligi yetu na nje ya ligi yetu etc.


Hizi ni sababu alizotaja Bocco na kuzielezea vizuri kwenye makala yake (soma tena makala hiyo), lakini katika maelezo yake amegusia mambo mengi ikiwemo kukosekana kwa mfumo wa soka la vijana, miundo mbinu mibovu ya mpira, waamuzi wabovu, viongozi wa kizamani, makocha wa kizamani ndani ya soka la nchi hii n.k.
Mengi aliyosema Bocco yanasemwa pia na makocha, wachambuzi na waandishi wa habari.  Elimu ya kutosha kuhusu namna ya kutengeneza mfumo wa soka la vijana, falsafa ya nchi, namna ya kutafuta makocha na wachezaji wa timu ya Taifa imeshatolewa sana , lakini kwa bahati mbaya viongozi wanaohusika wamekuwa wakipuuza maoni hayo  kwasababu wanaendesha soka kwa maslahi binafasi.
Kutokana na makala ya Bocco, nimeamua kumpongeza kwa moyo wote. Nimeona mara nyingi makala za wachambuzi na waandishi wenzangu na ninaendelea kuziona, lakini makala za wachezaji waliopo kwenye mpira kwasasa kama Bocco ni adimu mno.

Bocco ameniaminisha kuwa kuna wachezaji makini, wanajua vitu vingi, lakini wanashindwa kusema kwasababu wanawaogopa viongozi wao ambao hawapendi kuambiwa ukweli, wanaendekeza chuki, uzandiki na visilani. Je, kwa viongozi hawa, mchezaji akisema ukweli atacheza mpira? Sina hakika!.
Nigusie kidogo kuhusu makocha wazawa;  inawezekana kabisa makocha hawa  wamekuwa wagumu kujifunza vitu vipya. Kwa wanaotumia ‘Smartphone’ lazima wanakutana na jumbe za mara kwa mara zikiwataka ‘wa-update programs’ mbalimbali ndani ya simu zao.
Unapoambiwa ‘update  program’  maana yake kuna maboresho yamefanyika, wataalamu wanahangaika usiku kucha kuboresha na  kubuni vitu vipya. Hata katika soka, sheria kwa asilimia karibu zote zimeendelea kuwa zile zile, lakini kadri mpira unavyoendelea duniani, kumekuwa na maboresho ya sheria hizo ili kuendana na usasa.
Ndio maana waamuzi na makocha wa mbele wamekuwa wakijifunza kila kukicha, je, wakwetu Wana-update akili zao? Au bado wapo kwenye uzamani unaosemwa na  Bocco?
Binafsi naamini wapo wanaojifunza mbinu mpya kila siku na kuna wengine wamebaki kwenye uzamani. Ukienda kwenye program za mazoezi ya timu za ligi kuu, ligi daraja la kwanza utagundua kama makocha wetu wamebaki kwenye uzamani au wana usasa.
Kuna wengine wanaendana na usasa, ila kuna wengine wameendelea kufundisha mpira wa kizamani, kuna haja ya kubadilika katika hili.
Ishu nyingine niliyoguswa nayo ni waamuzi; Bocco anadai sio wazuri , wanachezesha kizamani na wakienda kucheza mechi za kimataifa wanakutana na waamuzi wazuri na wakisasa na ndio maana timu za Tanzania kwenye mashindano ya kimataifa zinapata kadi nyingi, offside nyingi, mwisho wa siku zinafungwa kwasababu walishazoeshwa vibaya na marefa wa ligi yetu.

Bocco anasisitiza kuwa huwezi kupata mchezaji mzuri wa Timu ya taifa  kutoka kwenye ligi mbovu isiyo na viwanja bora, mipira bora, uongozi bora, marefa bora wala mashabiki bora.

Amini usiamini! Bocco anayo siri kubwa sana kuhusu waamuzi! Kiukweli kuna madudu mengi yanayofanywa na waamuzi, wengine si kwa kupenda. Kuna rushwa inatembea vibaya mno. Sio kweli kwamba waamuzi wetu hawajui sheria za kisasa, wanajua sana kwasababu sheria hazibadiliki sana zaidi ya kuboreshwa.

Baadhi ya makosa ya makusudi wanayofanya  waamuzi ni maelekezo ya watu fulani, kuna waamuzi wanaondolewa kwenye ratiba ya mechi kadhaa kwasababu ya misimamo yao. Akikataa rushwa ili apange matokeo, basi utasikia wamefanya mabadiliko. Kuna watu wanataka mambo yao yatimie kidhuluma.

Nimejifunza mengi katika mechi za mwisho za ligi kuu soka Tanzania bara msimu 2014/2015 uliomalizika mei 9 mwaka huu.  Waamuzi wametumika mno, timu nyingine zimepata nafasi za juu kwasababu ya mipango, timu nyingine zimeshushwa daraja kidhuluma.

Bocco anajua haya, lakini hawezi kusema kiundani zaidi ya kusema waamuzi wanachezesha kizamani. Waamuzi wengine wana mapenzi na timu za Simba, Yanga, wanachezesha kiunazi, lakini waliowengi ni wala rushwa. Kinachouma zaidi ni kwamba; wanaohusika kupanga matokeo ni watu wanaoonekana makini mbele ya jamii.

Inashangaza sana kuona kiongozi mkubwa wa soka anatoa maelekezo Ruvu Shooting ashuke daraja kwa maslahi ya watu fulani, Yanga ipate  ushindi, Azam ipate ushindi au Mgambo wapewe pointi, Ndanda wabakishwe ligi kuu kwasababu za kisiasa. 
Waamuzi wanaelekezwa nini cha kufanya, akijifanya anapenda ‘Fair Play’ hapangwi kwenye mechi .

Waamuzi wanavuna mamilioni kwasababu ya rushwa, wanapiga vimeo vingi vya ligi kuu na kuendesha maisha. Wanajua wanachokifanya na wanaposoma hapa wanasutwa nafsi zao.

Kuhusu viongozi wa kizamani ni kweli kabisa. Kiongozi bora ni yule anayekubali kujifunza. Siku zote wanaojifanya wanajua wana-feli vibaya mno. Ulimwengu unabadilika, mambo yanabadilika kila siku, lazima ujifunze kwa wengine.

Kwa habati mbaya viongozi wengi wa soka kuanzia ngazi za chini mpaka TFF wanajifanya wataalamu wa soka, hawashauriki, wanaamini katika mawazo yao, hawajifunzi wala kupokea maoni ya  wengine, madhara yake wanafeli.

Hata kocha wa Taifa Stars, Mart Nooij anajiamini kupita maelezo, anajiona ndiye bora kuliko wote, lakini kama angekuwa bora angekuja kuganga maisha Bongo?

Kuna watu wa maana wapo nchi hii, wanajua mpira mno, wana uzoefu mkubwa, lakini huyu mzungu hata kuwasalimia na kubadilishana mawazo hataki, anaamini anaweza kuliko wote.

Hawezi hata kumpigia simu Hans van der Pluijm wa Yanga kujua hali ya kiafya ya Said Makapu, Nadir Haroub inaendeleaje.  Matokeo yake anachaguo hata wachezaji majeruhi kwenye kikosi cha timu ya taifa.

Nooij hawezi kuifikisha Tanzania popote kwasababu ya kiburi chake, Kim Paulsen alikuwa mtu wa watu, alipenda kujifunza, lakini Malinzi akamuondoa bila sababu za msingi.

Inawezekana kweli makocha wa ndani ni wa kizamani, lakini si kwa kiwango hicho. Kila siku tunasikia kozi za makocha na wakati mwingine wakufunzi wanatoka CAF na FIFA, makocha wetu wanajua sana, lakini hawathaminiwi.

Mtu mweupe ndiye bora, hivyo ndivyo tunaamini. Lakini ukweli ni kwamba Hans van der Plujim, Goran Kopunovic akikutana na Juma Mwambusi, Bakari Shime uwanjani, waamuzi wakawa ‘fair’ asilimia 100, utagundua kuwa hawana utofauti mkubwa katika uwezo wa kufundisha mpira.

Vitabu vya mpira ni vile vile, ndio maana hata mzungu mzaliwa wa Uingereza anaweza kufeli somo la kiingereza licha ya kuwa lugha yake mama. Kwa waliosoma na wazungu wana ushahidi wa kutosha, wanazidiwa na waafrika katika mambo mengi, lakini kwa bahati mbaya waafrika hatujikubali na hatukubaliki na waafrika wenzetu.

Kuna kocha yeyote mzungu amewahi kuja Tanzania katika ngazi ya klabu na kujaribu kusogelea rekodi ya Mfalme Abdallah Kibadeni pale Simba na Tanzania hii?

Huyu nidye kocha pekee aliyeifikisha Simba kwenye fainali ya kombe la CAF, siku hizi kombe la Shirikisho. Rekodi hiyo haijawahi kufikiwa wala kusogelewa na kocha yeyote awe mzungu au Mtanzania katika timu zote za Tanzania. Unaanzaje kumdharau Kibadeni? Ndiyo! Unaweza kusema ana uzamani kwa mtazamo rahisi tu, lakini ni kwamba yule ni mtu muhimu mno.

Bocco kaongea mengi, sijataka kurudia wala kuongeza. Lengo langu ni kumpongeza tu na kujaribu kugusia baadhi ya mambo aliyosema!

Hongera sana! John Raphael Bocco ‘Adebayor’ kwa kutueleza hisia zao na ukweli wa soka letu. Viongozi chukueni maoni yake, sio dhambi kuyafanyia kazi.


Ni halali yako kutoa maoni, kukosoa mtazamo huu binafsi!


Na Baraka Adson Mpenja


Mtangazaji wa mpira wa Miguu-Azam TV


Tel: 0712461976



0 comments:

 
voyeur porn porn movies sex videos hd porno video