Thursday, May 21, 2015

MLINZI na kiungo wa zamani wa Yanga na Taifa Stars, Ally Mayay Tembele ametoa maoni yake kuntu kufuatia timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars kufungashiwa virago katika michuano ya Cosafa inayoendelea Afrika kusini.
Stars ilifungwa goli 1-0 dhidi ya Swaziland katika mechi ya kwanza ya kundi B na jana ikafungwa 2-0 na Madagascar , sasa inasubiri kukamilisha ratiba kwa kucheza mechi ya tatu kesho dhidi ya Lesotho majira ya saa 12:00 kwa saa za Tanzania.
Ukiziangalia timu za Kundi B kwa maana ya Tanzania, Madagascar, Lesotho na Swaziland, Tanzania ndio nchi yenye kiwango cha juu katika viwango vya CAF na FIFA, lakini imekula ‘manundu’ katika mechi zake mbili.
Katika mahojiano maalumu na MPENJA BLOG, Ally Mayay ametoa maoni yake  ambayo tunakuletea kama yalivyo:
“Makocha kupingwa kwasababu ya uteuzi wa wachezaji fulani sio suala geni duniani. Watanzania sio watu wa kwanza kumlalamikia kocha kuwa,  kuna wachezaji fulani hawafai, makocha wengi hukutana na kadhia hiyo.
Kama unakumbuka mwaka 2002, kocha Luiz Felipe Scolari alipingwa mpaka na rais wa Brazil kwa kumuacha Romario da Souza, lakini alikwenda na kushinda kombe la dunia kule Korea kusini na Japan. Siku zote unapopingwa unatakiwa kupata matokeo, kama matokeo hayapatikani, hapo unawajibika kwa asilimia 100.
Kuanzia uchaguzi wa wachezaji wa Taifa Stars kumekuwa na maneno mengi, wadau wa soka wanapingana na uteuzi wa mwalimu Mart Nooij. Kilichotakiwa kwake ni kupata matokeo, sasa kwa bahati mbaya matokeo hajapata, dunia nzima inaelewa kwamba mwalimu atawajibika.
Mbaya zaidi  ni kwamba Nooij hana ushirikikiano na makocha wenzake kujua nini kinachoendelea, unajua wazi wachezaji wanalelewa na vilabu, akiwa mwalimu wa timu ya taifa anatakiwa kuwa na mawasiliano ya kila siku kujua hali za wachezaji, yeye anakaa na wachezaji siku tano, sita au saba, lakini wachezaji kwa mwaka mzima wanalelewa na makocha wa vilabu zao.
 Ndio maana Ulaya utakuta kocha Arsene Wenger anamwambia kocha wa timu ya taifa ya Uingereza, Roy Hodgson kwamba usimpange Theo Walcott kwasababu jana tu ndio ameanza mazoezi mepesi kwasababu alikuwa na majeruhi ya miezi miwili.
Kwahiyo kocha wa timu ya taifa  anafahamu hali ya Walcott iko vipi. Lakini ukija kwetu makocha wengi Wazungu hawana ushirikiano wa moja kwa moja na makocha wa vilabu hasa wazawa ambao wana wajibu mkubwa wa kujua wachezaji.
Kwa bahati mbaya Mart Nooij hana uhusiano mzuri na vyombo vya habari, lakini kwenye ile semina ya Wakufunzi wa soka iliyofanyika wiki mbili zilizopita pale TFF, Nooij alikuwa moja kati ya watoa maada.
Aliambiwa na mkurugenzi wa ufundi wa TFF, Mwalimu Salum Madadi kwamba waliopo mbele yako ni ‘Senior Coaches’. Ni makocha wa Kitanzania ambao wamefanya kazi katika vilabu mbalimbali na wengine timu ya taifa kwa muda mrefu, alichojibu hakuonesha kabisa kama anataka hata kubadilishana mawazo na makocha wazawa, alisema yeye alikuja na begi lake, ataondoka na begi lake, hii inaashiria kile kinachotokea sasa hivi.
Anaweza kuchagua mchezaji, halafu siku mbili akapanda ndege kurudi nyumbani kwasababu ya majeruhi (Juma Said Makapu), hii ni kwasababu hana mahusiano ya moja kwa moja na makocha wa vilabu, unamchagua Haruna Chanongo kumbe alishaumia siku mbili zilizopita,  pia akina Nadir Haroub, Aishi Manula, Hassan Isihaka wote walikuwa na majeruhi lakini aliwachagua. Hii ni kasoro kubwa, miongoni mwa vitu ambavyo makocha wanatakiwa kuwa navyo na ni sifa kubwa ya kuwa kocha bora ni kujifunza kila kitu.
Kama kocha hutaki kujifunza basi unapoteza sifa ya kuwa kocha bora.  Bahati mbaya sana Mart Nooij anakutana na kadhia hiyo kutokana na kile anachosimamia. Huwezi kusema tunakwenda Sauzi Afrika kama mazoezi ya kucheza mechi za kufuzu kwa CHAN na AFCON, hata kama tunakwenda kujifunza ndio tuporomoke?.
Tunatakiwa kujifunza huku tukilinda heshima yetu, tunakwenda kushiriki kwenye michuano huku tukionekana sisi ndio wenye nafasi kubwa katika timu za kundi B, yaani kwenye kundi letu sisi ndio wenye kiwango bora zaidi, Swaziland waliotufunga wako nafasi ya 46, sisi tuko nafasi ya 30 kati ya mataifa 54 ya CAF,  hawa Madagascar wako nafasi ya 43.
Hata kama tumepoteza, tumepotezaje? Timu inaonekana haina mpangilio kuanzia inavyocheza, mpango wa mechi ya kwanza ndio huo huo mechi ya pili, tunafungwa magoli ya aina moja ya kushitukiza.
 Hii ni kengele kwa wanaosimamia mpira, wanatakiwa kuuliza wataalamu wa mpira, wasikae wakajifungia vyumbani kwamba wao tu ndio wanajua mpira, sio wao tu wanaojua mpira, tuna makocha wakubwa wazawa waliofundisha mpira kwa zaidi ya miaka 30, wanatakiwa kuwauliza maoni yao na wayajumuishe katika shughuli za kuendeleza soka”,

Huo ndio mtazamamo wa Ally Mayay….unayo nafasi ya kutoa maoni yako pia….

0 comments:

 
voyeur porn porn movies sex videos hd porno video