Sunday, January 18, 2015

Kocha wa Mbeya City fc, Juma Mwambusi ambaye ni kocha bora wa Msimu uliopita

KUNA msemo maarufu uliotumika sana mwaka jana usemao: “Jiamini, jitathimi na jiongeze” .

Kujiamini kwa kila jambo unalofanya ni silaha ya mafanikio, lakini lazima uwe unajitathimini kila baada ya muda ili kuona umefanikiwa kiasi gani na umekwama wapi, halafu unajiongeza kwa kutafuta njia mbadala na kuongeza juhudi zaidi ili kufikia malengo yako.

Mbeya City walianza ligi vibaya msimu huu tofauti na msimu wa mwaka jana. Kumbukumbu zinaonesha mechi ya kwanza iliyopigwa septemba 20 mwaka jana walitoka suluhu (0-0) dhidi ya Maafande wa JKT Ruvu katika uwanja wa Sokoine Mbeya.

Mechi ya pili waliifunga Coastal Union bao 1-0. Bao hilo la penalti lilifungwa na Deogratius Julius. Kipute hicho kilipigwa uwanja wa Sokoine septemba 27 mwaka huu.

Baada ya mechi hiyo Wagonga Nyundo hao wa Mbeya wakasafiri kwenda Matabini Mlandizi, Pwani ambapo walitoka suluhu (0-0) na wenyeji wao Ruvu Shootings.

Suluhu mbili na ushindi katika mechi tatu za kwanza hayakuwa matokea mabaya kimpira, lakini watu wengi wakaanza kuhoji kiwango cha Mbeya City wakiamini kimeshuka kufananisha na msimu uliopita ambapo walitikisa nchi kwa kandanda murua.

Balaa lilianza kuwaangukia ‘Wanyampara’ hao wa Mbeya katika mechi ya nne ambapo walifungwa goli 1-0 na Azam fc katika uwanja wao wa nyumbani, hii ilikuwa Oktoba 18 mwaka jana. Nakumbuka bao hilo lilifungwa kwa mpira wa adhabu ndogo na nahodha msaidizi wa Wanalambalamba, Aggrey Morris.

Kipigo hicho hakikuwashitua wengi kwasababu Azam walikuwa na rekodi ya kupata matokeo uwanja wa Sokoine na moja ya chachu ya ubingwa wao msimu uliopita ilikuwa ushindi wa 2-1 waliovuna dhidi ya City katika uwanja huo.

Kufuatia kipigo hicho, minong’no ikaendelea na Oktoba 26, Mbeya City ikafungwa mabao 2-0 na Mtibwa Sugar katika uwanja wa Nyumbani.

Kipigo hicho kilizidi kutibua rekodi ya City ya kubana katika uwanja wake. Kilikuwa kipigo cha tatu katika historia ya klabu hiyo kwenye michuano ya ligi kuu.

Kikosi cha Mbeya City fc

Wakiwa katika maumivu hayo, City walisafiri kwenda Tanga, Novemba 2 mwaka jana kucheza na Mgambo JKT ambapo walifungwa mabao 2-1.

Kutoka Tanga pengine wakadhani wataifunga Stand United Oktoba 8 mwaka jana katika uwanja wa CCM Kambarage Shinyanga, lakini wakaambulia kipigo cha bao 1-0.

City walimaliza raundi ya 7 ya  ligi kuu wakiwa na pointi 5 katika nafasi ya mwisho ya msimamo.

Matokeo haya yaliwaumiza viongozi, wachezaji na mashabiki wa timu hiyo pendwa nchini.

Wakati wa mapumziko ya mwezi mmoja na zaidi kulizuka taarifa za klabu hiyo kuachana na kocha Juma Mwambusi na yeye mwenyewe alitangaza kujiuzulu kazi yake akidai amechoshwa na maneno ya watu kutokana na matokeo mabaya.

Uongozi wa klabu ulikaa na kocha huyu bora wa msimu uliopita na kumaliza tatizo na hatimaye akaendelea na kazi ya kusuka kikosi chake.

Kama unajua mpira, tatizo kubwa la Mbeya City lilikuwa katika safu ya ulinzi, ndani ya mechi saba iliruhusu nyavu zake kuguswa mara 6. Safu ya kiungo na ushambuliaji pia haikuwa na makali.

Mwambusi aliongeza wachezaji kadhaa katika dirisha dogo akiwemo beki kisiki Juma Said Nyosso.

Nyosso, beki wa zamani wa Simba, Coastal Union na Taifa Stars siku zote anajua kazi yake na amekuwa mjanja sana anapokuwa katika  eneo la ulinzi.

Usajili huo umewafanya Mbeya City wacheze mechi mbili za ligi bila kufungwa goli. Walishinda 1-0 dhidi ya Ndanda fc desemba 28 mwaka huu uwanja wa Sokoine na jana wameibuka na ushindi wa kwanza ugenini msimu huu kwa kuifunga Kagera Sugar 1-0 uwanja wa CCM Kirumba.

Katika mechi hiyo niliangalia mambo mawili makubwa, moja ni namna kocha Mwambusi alivyojenga upya kikosi chake kimbinu na kiufundi pamoja na nidhamu ya mchezo kwa wachezaji.


Mashabiki wa Mbeya City fc kwenye moja ya mechi ya timu hiyo uwanja wa Sokoine Mbeya

Pili nilijikita zaidi kuona namna mashabiki wanavyoiunga mkono timu yao.

Jambo la kwanza, niligundua Mbeya City wamebadilika, wamekuwa kwenye kiwango kizuri. Walicheza vizuri safu ya kiungo na ulinzi.

Mabeki wa pembeni John Kabanda (kulia) na Hassan Mwasapili (kushoto) walikuwa wanakaba vizuri katika nafasi zao, walijitahidi kupandisha timu na nidhamu yao ilikuwa juu. Walijua wakae wapi, wafanye nini kuwazuia mawinga wa Kagera Sugar. Walifanikiwa kwa kiwango kikubwa na kuwafanya Juma Nyosso na Yusuph Abdallah wawe na kazi rahisi katikati.

Nyosso na mwenzake hawakuwa na kazi kubwa ya kwenda kuwasaidia mabeki wa pembeni, walikuwa na uhakika na Kabanda na Mwasapili. Safu ya ulinzi ilicheza vizuri sana.

Pia akina Nyosso walikuwa bora kutokana na kiungo wa ulinzi Steven Mazanda na mwenzake Rafael Daud kulimudu dimba la kati.

Viungo walicheza pasi rahisi, fupi na pasi ngumu kuwafikia viungo washambuliaji ambao waliongozwa na Cosmas Fredy aliyecheza nyuma ya Paul Nonga.

Them Felix aliyeanzia kulia, huku Deus Kaseke akiwa kushoto walicheza vizuri na kufika mara nyingi eneo la mwisho la Kagera Sugar na isingekuwa umakini wa mabeki wa wakata miwa hao,wangefungwa magoli mengi.

Mbeya City fc walikuwa na kasi nzuri, walicheza vizuri wanapomiliki mpira na cha kufurahisha zaidi walijitahidi kukaba vizuri wanapopoteza mpira.

Jambo la pili nililoliona ni amsha amsha za mashabiki kwa muda wote. Hawa ni mashabiki ninaowafahamu mimi. City wamefanikiwa kuwa na mashabiki wa kweli.

Hawa watu wanaipenda sana timu yao, walikuwa zaidi ya 200 uwanja wa CCM Kirumba. Lugha ya miili yao ilionesha wanaipenda timu yao na hawaoni shida kupoteza pesa kusafiri kwenda popote pale nchini.

Unapocheza mpira halafu kuna watu wengi nyuma yako wanakusapoti hata kama ulikuwa na matokeo mabaya nyuma, kunaongeza morali kubwa.

Siku zote mashabiki ni mchezaji wa 12, mchezaji wa uwanjani hana uwezo wa kuwalipa mshahara kwa kushangiliwa, fadhila pekee wanazopokea ni wachezaji kuucheza mpira kwa kiwango cha juu.

Wachezaji wa Mbeya City, viongozi na benchi la ufundi, jikumbusheni kuwa kuna watu wengi wapo nyuma yenu. Mna wajibu mkubwa wa kuifanya timu iwe bora.

Kinachotakiwa kufanyika ni kuifanya timu iwe bora muda wote ili kurudisha fadhila kwa mashabiki. Mpira una matokeo matatu, kufunga, kufungwa na kutoa sare.

Matokeo yoyote yanayopatikana ni sawa katika mpira, lakini linapokuja suala la kiwango cha timu lazima lionekane wakati wote.

Sina shaka na uwezo wa kocha Mwambusi kimbinu na kiufundi, lazima apewe sapoti kubwa ili kuendeleza mazuri aliyokuwa nayo.


Siku njema!

0 comments:

 
voyeur porn porn movies sex videos hd porno video