Kikosi cha Simba kilichoanza leo
WEKUNDU wa Msimbazi wamefanikiwa kufuzu hatua ya
robo fainali ya kombe la Mapinduzi kufuatia kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi
ya vinara wa ligi ya Zanzibar, JKU katika mechi iliyomalizika usiku huu uwanja
wa Amaan Zanzibar.
Bao pekee la Simba limefungwa na Ramadhani Singano
‘Messi’ katika dakika ya 11 kwa shuti kali akipokea pasi murua ya Said Ndemla.
Kwa matokeo hayo, Simba wameibuka vinara wa kundi
C kwa kujikusanyia pointi 6 kibindoni, huku nafasi ya pili ikishikwa na Mtibwa
Sugar wenye pointi tano.
Kikosi cha Simba kilichoanza leo
Simba walianza mchezo kwa kasi, lakini JKU walionekana
kuchakarika kuwadhibiti wakali hao wa Msimbazi.
Kikosi cha Mnyama kinachonolewa na Mserbia Goran
Kopunovic kimeonekana kucheza mpira wa kasi na pasi za uhakika kuanzia sehemu
ya ulinzi na safu ya ulinzi.
Baada ya mechi hiyo, kocha Kopunovic amesema timu
yake inaimarika kidogo kidogo na ilicheza tofauti kwa vipindi vyote.
“Hii ni siku ya tano tu tangu nifike, bado
naendelea kuwapa mbinu mpya. Wachezaji wangu kimbinu nawaona wazuri”
“Mimi napenda vijana ndio maana nawatumia wengi.
Kidogo kidogo tutakuwa safi” Alisema Kopunovic.
Simba wanasubiri mpinzani wao wa Robo fainali katika
mechi za kesho ambapo kutakuwa na mechi nne.
Majira ya saa 9:00 alasiri katika uwanja wa Amaan,
KCC watachuana na KMKM, saa 11:00 jioni Azam fc watakabiliana na Mtende, hizo
ni mechi za kundi B.
Kundi A, Taifa ya Jang’ombe itapepetana na Polisi
katika uwanja wa Mao Dze Tung majira ya saa 9:00 alasiri.
Mtanange mwingine wa kundi A utawakutanisha Yanga
dhidi ya Shaba majira ya saa 2:00 usiku uwanja wa Amaan.
0 comments:
Post a Comment