Tuesday, January 13, 2015

KAMA mikwara ya nje ya uwanja ni ubingwa, basi Simba ni bingwa wa Kombe la Mapinduzi hata kabla ya fainali ya leo Jumanne usiku dhidi ya Mtibwa kwenye Uwanja wa Amaan hapa Unguja, Zanzibar.
Simba ambayo ina uzoefu na mechi zaidi za fainali kuliko timu yoyote nchini, imebadilika ndani na nje ya uwanja baada ya kufuzu hatua hiyo.

Tangu wikiendi iliyopita, viongozi wote wa juu wa Simba pamoja na wajumbe wa kamati zake, wamehamia karibu na kambi ya timu yao mjini hapa na kumekuwa na vikao vya mara kwa mara na wachezaji pamoja na kocha katika kuhakikisha wanazima kiburi cha Mtibwa ambayo katika siku za hivi karibuni imekuwa ikiitesa Simba kwenye michezo ya ligi na ile ya kirafiki.

Simba wamepandwa na mzuka hasa baada ya Yanga na Azam kung’olewa kwenye michuano hiyo ambayo waliokuwa mabingwa mtetezi KCCA ya Uganda walitolewa hatua ya robo fainali.

Habari za ndani zinadai kwamba vigogo watatu wa klabu hiyo wamevuka mipaka kwa kumpa kocha mpya, Goran Kopunovic kikosi ambacho wanataka kianze jambo ambalo vibosile wengine wakiongozwa na Rais Evans Aveva wamelikemea vikali na kumtaka kocha kutotoa ruhusa kwa watu kuingilia kazi zake.

Mashabiki wa Simba wameanza kumwagika kwenye viunga vya Zanzibar tangu juzi Jumapili jioni na jana Jumatatu bendera za rangi nyekundu zilitawala maeneo mengi ya Unguja ingawa Mtibwa nao walikuwa wajanja kwa kufanya mazoezi na programu zao sirini sana.

Mchezo huo utakaoanza saa 2:15 usiku, utazikutanisha timu zenye historia tofauti katika michezo mbalimbali ya fainali ambayo wameshinda mara 15 wakipoteza mara 7.

Wekundu hao wamecheza fainali za Mapinduzi mara nne na kuchukua mara mbili wakizifunga Mtibwa mwaka 2008 na 2011 wakiwafunga Yanga 2-0 huku wakipoteza dhidi ya Azam kwa mabao 2-1 mwaka 2012 na mwaka jana Mnyama alichapwa na KCCA mabao 2-0.

Mbali na mashindano hayo makali ya Simba katika mechi za fainali pia yalionekana katika Kombe la Kagame ambalo walichukua mara 6 ambazo ni nyingi kuliko klabu yoyote ya Tanzania hata Afrika Mashariki yote.

Rekodi za Simba kwenye fainali pia zinaonyesha Simba ilichukua kombe katika mechi za Kombe la Nyerere miaka ya 1984,1995,2000. Mtibwa wameingia fainali ya mapinduzi mara mbili miaka ya 2007 alifungwa na Yanga na 2008 ambapo walifungwa na Mnyama.

Mwaka 2009 ilichukua Kombe la Tusker dhidi ya URA ya Uganda, pia Mtibwa ikalichukua tena kombe hilo mwaka 2010 kwa kuifunga Ocean View, pia wamewahi kuingia fainali ya Kombe la ABC Bank mara moja na kufungwa na Simba mabao 3-2.

Simba iliyoweka kambi katika eneo lao la Mbweni Unguja na ikijifua katika Uwanja wa Chuo cha Ualimu Chukwani, itaingia uwanjani ikiwa na kikosi tofauti na kile kilichokubali kipigo cha bao 1-0 dhidi ya Mtibwa katika mechi ya kwanza ya hatua ya makundi.

Hiyo ni kutokana na kuwasili kwa nyota wake wawili; Simon Sserunkuma na Emmanuel Okwi.

Ikiwa chini ya kocha Mserbia Kopunovic, Simba imekuwa ikiongeza dozi ya mazoezi yake ambapo tangu ikijiandaa na mechi ya nusu fainali timu hiyo imekuwa ikifanya mazoezi makali mara mbili kwa siku huku kocha huyo akitamka kwamba sasa timu yake ipo tayari kwa pambano.

“Kichwani kwangu kuna mambo mawili muhimu, kwanza maandalizi ya ligi ambayo ndiyo muhimu kwetu lakini la pili ni hii mechi ya kesho (leo Jumanne) ambayo endapo tutachukua ubingwa utakaotusaidia kuingia katika mechi za ligi tukiwa na morali mpya,”alisema Kopunovic.

“Bado hatujapata uhakika wa kumtumia Simon Sserunkuma, anaonekana kuwa na maumivu lakini kila kitu tutajua kesho (leo) endapo atakuwa bado na maumivu hatutamtumia, sitaki kumpa madhara makubwa kwa ajili ya mchezo huu kwa kuwa sasa tunaye Okwi,”alisisitiza kocha huyo.

Mtibwa yashtukia ishu

Mtibwa imehofia hujuma zozote zinazoweza kufanywa dhidi ya wachezaji wake na ilichofanya ni kutibua ratiba zake za mazoezi ili kuichanganya Simba.

Mtibwa ambayo kwa msimu huu tayari imeshaifunga Simba mara mbili na kutoka nayo sare moja, imejipanga kuhakikisha inaendeleza rekodi yake hiyo ambapo katika maandalizi yake imelazimika kufanya mazoezi kwa siri kubwa.

Timu hiyo inayofundishwa na kocha mzalendo, Mecky Maxime, iliuanza msimu huu ikipata sare na Simba katika mechi ya Ligi Kuu Bara iliyopigwa mjini Morogoro na baadaye kuibuka na ushindi wa mabao 4-2 katika mchezo wa kirafiki uliopigwa katika Uwanja wa Chamazi kabla kuishinda tena Simba bao 1-0 katika hatua ya makundi ya Kombe la Mapinduzi.

“Tunawaheshimu Simba, haina maana kwamba tulipowafunga mchezo ule ulikuwa mteremko, tumeshasahau matokeo yaliyopita sasa tunaanza upya,” alisema Maxime.

Mshindi kukabidhiwa kombe jipya

Kamati ya Maandalizi ya mashindano hayo kupitia Katibu wake Hamis Abdallah, imesema kuwa mshindi wa mchezo huo ambao mgeni rasmi atakuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dr. Ali Mohamed Shein, mbali ya donge la na Sh10 milioni, pia atapatiwa kombe jipya tofauti na lile lililobebwa na mabingwa waliopita KCCA ya Uganda na medali za dhahabu

Mshindi wa pili atajizolea Sh5 milioni bila kombe na medali za shaba kwa wachezaji wote 25 huku pia kukiwa na zawadi kwa mfungaji bora, kipa bora na mchezaji bora wa mashindano hayo

Phiri ashauri

Kocha wa Simba aliyepigwa chini, Mzambia Patrick Phiri, ameitakia kila la kheri timu hiyo katika fainali za Kombe la Mapinduzi zitakazochezwa leo Jumanne usiku, lakini ametahadharisha kwamba wasipokuwa makini wanaweza kufungwa na Mtibwa.

Akizungumza na Mwanaspoti kutoka Zambia, Phiri alisema: “Mtibwa ni wazuri sana, lakini katika soka hiyo haijalishi sana kwani inaweza kuwa nzuri na ikafungwa, kikubwa Simba watulie ili washinde mechi hiyo vinginevyo ubingwa utaenda Mtibwa, nawajua Mtibwa kwani nimekutana nao kwenye ligi na mechi ya kirafiki.”


Phiri hakuacha kuwazungumzia wachezaji wake nyota, Waganda Emmanuel Okwi na Joseph Owino ambaye anatarajia kurejea nchini muda wowote wiki hii.


“Nafurahi kusikia Okwi yupo kambini na timu, ni mchezaji mzuri ila anatakiwa kubadilika sasa, amekuwa mkubwa, anatakiwa kuwa na nidhamu ili aendelee kuwa nahodha, Owino ni mchezaji muhimu kwenye timu, viongozi watatue matatizo yake kwa kipindi, najua tofauti zilizopo kati ya Owino na viongozi, ligi bado ngumu na uwepo wake unahitajika.”

Mgosi atishia nyau

STRAIKA wa Mtibwa Sugar, Mussa Hassan ‘Mgosi’ amesema endapo atashindwa kuifunga Simba kwenye mchezo wa fainali utakaochezwa Uwanja wa Amaan Zanzibar leo Jumanne, basi washambuliaji wenzake Ally Shomary na Ame Ally lazima watafunga kwenye mchezo huo.

“Tumejipanga kutwaa ubingwa wa Mapinduzi, hatutazembea nafasi yoyote tutakayoipata kwenye mchezo wetu na Simba, tutacheza kama timu kuhakikisha tunapata matokeo,” alisema straika huyo.

“Nisipowafunga mimi najua wenzangu watawafunga, safu yetu ya ushambuliaji ni nzuri na tumekuwa tukicheza kama timu kwa muda mwingi, hatuchezi kuangalia mtu mmoja anafanya nini, hata hivyo beki ya Simba haijabadilika sana tangu tulipocheza nayo mechi ya mwisho.”



Source: Mwanaspoti

0 comments:

 
voyeur porn porn movies sex videos hd porno video