MABINGWA wa zamani wa Tanzania mara mbili
mfululizo, 1999 na 2000, Mtibwa Sugar ya Morogoro wametinga fainali ya michuano
ya Mapinduzi mwaka 2015 kufuatia kuitandika JKU ya Zanzibar penalti 4-3.
Mshindi alilazimika kupatikana kwa penalti baada
ya timu hizo kushindwa kufungana ndani ya dakika 90.
Mpaka kufikia dakika ya 9 kipindi cha kwanza,
Mtibwa Sugar walifanikiwa kupiga shuti moja lililolenga lango, wakati JKU wao
hawakuweza kupiga shuti lolote.
Dakika ya 28, Ally Shomari iliinyima Mtibwa bao la
kuongoza akipiga nje mpira wa krosi uliochongwa kutoka winga ya kushoto na
David Charles Luhende.
Dakika moja baadaye, JKU walifanya shambulizi zuri,
lakini shuti la mshambuliaji hatari Amour Omary ‘Janja’ lilipaa nje ya lango.
JKU waliendelea kufanya mashambulizi na katika
dakika ya 32 Mohammed Abdallah kutoka winga ya kushoto alipiga shuti kali
lililotemwa na kipa Said Mohamed wa Mtibwa na mpira kumkuta Mohammed Faki
aliyeshindwa kufunga akiwa yeye na goli, hatimaye Salim Hassan Mbonde akaosha
mpira.
Mtibwa waliendelea kuwa katika wakati mgumu kwani
dakika ya 40, Andrew Vicent alishindwa kucheza mpira mrefu uliopigwa
kutoka katikati na ‘Janja’ akaunasa,
lakini shuti lake la mguu wa kushoto lilipanguliwa na Kipa Said Mohammed.
Dakika ya 45, Ally Shomari alipenyeza pasi nzuri
iliyomkuta Ame Ally aliyeachia shuti lililowababatiza mabeki wa JKU na kuwa
kona.
Hata hivyo kona
hiyo iliyochongwa na Luhende haikuweza kuzaa matunda.
Mpaka dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika
hakuna timu iliyoweza kuona lango la mwenzake.
Kwa ujumla katika kipindi cha kwanza hususani
dakika 20 za mwisho, JKU walicheza vizuri kuanzia eneo la katikati na
kutengeneza nafasi nyingi, lakini washambuliaji wake wakiongozwa na ‘Janja’
hawakuwa na macho ya kuliona lango la Mtibwa.
Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kushambuliana
kwa zamu, lakini washambulizi wa timu zote hawakuwa na mipango sahihi.
Katika dakika ya 82 Ramadhan Kichuya alikosa goli
la wazi akipaisha mpira wa krosi uliochongwa na Vicent Barnabas aliyeambaa
winga ya kushoto akipokea mpira mrefu wa Salim Mbonde.
Katika dakika za mwisho, Mtibwa Sugar walipata
kona tatu mfululizo, lakini hazikuzaa matunda kutokana na umakini wa kukaba wa
mabeki wa JKU.
Mpaka dakika 90 zinamalizika timu hizo zilitoka
suluhu pacha ya bila kufungana na kulazimika kupigwa mikwaju ya penalti.
Wakati huo huo kamati ya mashindano ya kombe la
Mapinduzi 2015 imemtangaza mlinda mlango wa JKU, Mohammed Abdulrahman kuwa
mchezaji bora wa mechi hiyo ya kwanza ya nusu fainali.
Waliopata penalti kwa upande wa Mtibwa Sugar ni
Ally Lundenga, Henry Joseph, Ramadhani Kichuya na Vicent Barnabas, wakati
Luhende alikosa mkwaju wake.
Waliofunga kwa upande wa JKU ni Isihaka Othman,
Issa Khaidari, na Khamis Abdallah, wakati Ismail Khamis alikosa tuta lake.
Mtibwa Sugar wanamsubiri mshindi atakayepatikana
katika mechi inayotarajia kupigwa usiku huu baina ya Simba na Polisi.
0 comments:
Post a Comment