MTIBWA Sugar wameirudisha Azam fc jijini Dar es
salaam kuendelea na maisha mengine baada ya kuwatandika penalti 7-6 Wanalambalamba
hao wa Chamazi katika mchezo wa tatu wa robo fainali ya kombe la Mapinduzi uliomalizika
dakika chache zilizopita uwanja wa Amaan mjini Zanzibar.
Ililazimika kutumia mikwaju ya penalti ili kumpata
‘kidume’ kufuatia timu hizo kutoka sare
ya 1-1 katika muda wa kawaida.
Bao la Mtibwa lilofungwa na Ally Shomari dakika ya
63 , lakini Kipre Tchetche aliizawazishia Azam katika dakika ya 89.
Robo fainali ya pili ya michuano hiyo iliyotangulia
mapema baina ya KCC na Polisi zilipigwa penalti 14, lakini hii ya tatu imetandikwa mikwaju 16, kila timu ikipiga
mikwaju nane.
Waliofunga penalti kwa upande wa Mtibwa Sugar ni
Shabaan Nditi, Henry Joseph, David Charles Luhende, Vicent Barnabas, Musa
Nampaka, Mzamiri Yasin na Said Mkopi, wakati Ame Ally penalti yake ilidakwa na
Aish Manula.
Waliofunga penalti kwa upande wa Azam fc ni Aggrey
Morris, Didier Kavumbagu, Erasto Nyoni, Brian Majwega, Jonh Bocco ‘Adebayor’ na
Pascal Wawa. Waliokosa ni mfungaji wa goli la kusawazisha, Kipre Tchetche na
kipa Aishi Manula.
Bao la Mtibwa Sugar, mabingwa wa zamani wa
Tanzania mara mbili mfululizo, 1999 na 2000 lilifungwa katika dakika ya 63 na
Ally Shomari Sharrif akimalizia mpira uliopigwa na Mshambuliaji wa zamani wa
JKT Ruvu, Simba na DC Motemapembe ya DR Congo, Musa Hassan ‘Mgosi’.
Kuingia kwa bao hilo kuliwafanya Mtibwa wacheze
kwa uangalifu mkubwa ili kulinda goli lao, huku Azam fc wakilisakama lango lao
wakihitaji kusawazisha.
Katika dakika ya 80, Mganda Brian Majwega alipiga
mpira wa adhabu ndogo ulioingia chumbani kwa Mtibwa na kupigwa kichwa na nahodha
Jonh Bocco ‘Adebayor’ , mpira ukadunda chini na kugonga mtambaa panya na kurudi
uwanjani na ndipo beki Pascal Wawa akapaisha mpira juu katika harakati za kutaka kufunga.
Wakati mashabiki waliofurika uwanjani wakiamini
Mtibwa Sugar wamesonga mbele, dakika ya 89 mshambuliaji wa Azam, Muivory Coast,
Kipre Herman Tchetche aliisawazishia timu yake kwa shuti kali akiunganisha krosi
ya Salum Abubakar ‘Sure Boy’.
Hilo ni bao la kwanza kwa Kipre katika michuano
hii ambaye hakucheza mechi tatu za mwanzo kutokana na kusumbuliwa na majeruhi.
Dakika 90 zilimalizika kwa sare ya 1-1 na ndipo
kanuni ya mikwaju ya penalti ikatumika.
Wakati huo huo, Kamati ya kombe la Mapinduzi 2015
ilimtangaza Salim Mbonde wa Mtibwa Sugar kuwa mchezaji bora wa mechi na
alikabidhiwa king’amuzi cha Azam TV.
Mtibwa Sugar wanasubiri mpinzani wao wa nusu
fainali katika mechi ya robo fainali ya mwisho inayotarajia kuanza dakika
chache zijazo uwanja wa Amaan baina ya Yanga na JKU.
0 comments:
Post a Comment