Wachezaji wa Simba wakimpongeza Ibrahim Haji 'Mido' (wa pili kulia aliyepiga magoti) kufuatia kupiha 'Hat-trick'
Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
WEKUNDU wa Msimbazi Simba wametinga kwa kishindo
hatua ya nusu fainali ya kombe la Mapinduzi 2015 kufuatia ushindi wa mabao 4-0
dhidi ya Taifa ya Jang’ombe uwanja wa Amaan Zanzibar usiku huu.
Ibrahim Hajib amefunga mabao matatu ‘hat-trick’ katika dakika ya 46, 62 na
75, wakati bao la nne limefungwa na Shaban Kisiga katika dakika ya 80.
Mapema kipindi cha kwanza Simba walianza kucheza mpira wa polepole wakigongeana
pasi za uhakika na kufika eneo la hatari la wapinzani wao, lakini Maguli na
Sserunukama walishindwa kujipanga vizuri na kupoteza nafasi nzuri za kufunga
magoli.
Kiungo wa ulinzi, Jonas Mkude alipiga pasi rahisi
na fupi fupi kwa viungo washambuliaji wa Simba
na mawinga wa pembeni na kuwafanya Simba wasogee zaidi eneo la hatari
wapinzani.
Mabeki wa pembeni, Mohammed Hussein (kushoto) na
Hassan Ramadhan Kessy (kulia) walipandisha timu na kupiga krosi, lakini bado
washambuliaji wa kati hawakuwa na mipango mizuri.
Simba walitengeneza nafasi nyingi, lakini walikuwa
na tatizo la umaliziaji.
Maguli alionekana kucheza chini ya kiwango,
akishindwa kumiliki mpira vizuri na kupiga mashuti, lakini kocha Kopunovic
aliendelea kumwacha mpaka kipindi cha kwanza kinamalizika.
Hata hivyo, Simba walijitahidi kupiga mashuti
yaliyolenga lango na mpaka kipindi cha kwanza kinamalizika walikuwa wamepiga
mashuti matano dhidi ya mawili ya wapinzani wao.
Katika kipindi hicho cha kwanza, Simba walimiliki
mpira kwa asilimia 57 dhidi ya 43 za Taifa ya Jang’ombe.
Katika kipindi cha pili, Simba walianza kwa
kushambulia lango la Taifa wakitafuta
bao la kuongoza.
Mapema dakika ya 46, Simba waliandika bao la
kuongoza kupitia kwa Ibrahim Ajibu kufuatia kuukuta mpira eneo la hatari baada
ya purukushani ya mabeki wa Taifa ya Jang’ombe na Danny Sserunkuma ambapo
alipiga shuti lililozama nyavuni.
Purukushani hiyo ilitokana na pasi iliyopigwa na
Kessy kwa Saimon Sserunkuma aliyempatia pasi ndugu yake Danny ambaye alipambana
na mabeki wa Taifa na mpira kumkuta Ajibu akiwa eneo zuri.
Dakika ya 62 almanusura aandike bao la pili
akijaribu kumalizia krosi ya Simon, lakini mlinda lango wa Taifa, Karim Musa aliokoa
na kuwa kona.
Katika dakika hiyo hiyo, Ajibu aliandika bao la
pili kwa shuti akimalizia mpira wa kona uliochongwa na Simon.
Dakika ya 73 Ajibu alimpiga chenga Hassan Soud eneo
la hatari akielekea kufunga, lakini Abdallah Haji akamuangusha na mwamuzi
akaamuru mkwaju wa penalty.
Akiwa tayari ana mabao mawili, Ajibu alikwenda
kupiga mkwaju huo wa penalti katika Dakika ya 75 na kufanikiwa kufunga bao safi
na kuandika ‘hat-trick’ ya pili katika mashindano hayo baada ya ile ya Saimon
Msuva.
Msuva alifunga mabao matatu peke yake katika mechi
ya ufunguzi ya kundi A Yanga ikishinda mabao 4-0 dhidi ya Taifa Jang’ombe.
Dakika ya 80, Shaban Kisiga aliifungia Simba bao la nne kwa mpira wa adhabu ndogo
baada ya Mohammed Hussein kufanyiwa madhambi.
Mechi nyingine tatu za robo fainali zitapigwa
kesho uwanja wa Amaan Zanzibar.
Mechi ya mapema itaanza saa 9:00 alasiri ambapo
KCC watachuana na Polisi Zanzibar.
Azam fc watashuka dimbani majira ya saa 11:00
jioni kucheza robo fainali ya tatu katika uwanja wa Amaan dhidi ya Mtibwa
Sugar.
Mechi ya mwisho itapigwa majira ya 2:15 usiku
ambapo Yanga wataoneshana kazi na JKU ya Zanzibar.
0 comments:
Post a Comment