Kocha mpya wa Simba sc
KIUNGO mshambuliaji wa Simba, Awadh Issa Juma
amekiri wazi kuwa kocha mpya wa timu hiyo, Mserbia, Goran Kopunovic ameleta
mbinu mpya katika timu yao.
Awadh aliyasema hayo baada ya Simba kufuzu robo
fainali ya kombe la Mapinduzi kufuatia kuitandika JKU bao 1-0 katika mchezo
uliopigwa uwanja wa Amaan usiku wa jana.
Bao hilo pekee lilifungwa kwa shuti kali na
Ramadhan Singano ‘Messi’ katika dakika ya 11 ya kipindi cha kwanza akimalizia
pasi nzuri ya Said Ndemla.
Katika mechi ya kwanza, Simba walifungwa bao 1-0
na Mtibwa Sugar, mechi ya pili wakashinda 1-0 dhidi ya Mafunzo na ushindi wa
jana umewafanya wajikusanyie pointi 6 na kuibuka vinara wa kundi C.
Awadh alisema kwasasa wanafanya mazoezi magumu kwa
lengo la kutafuta nguvu na kasi, hivyo watarudi vizuri ligi kuu.
“Kila kitu kimebadilika. Mwalimu amekuja na mbinu
mpya. Kwasasa tupo katika mazoezi magumu, ndio maana tulianza kwa kasi kipindi
cha kwanza, lakini kipindi cha pili kasi ilipungua”. Alisema Awadh.
“Tumempa muda mwalimu na tunaamini atatufikisha
mbali katika michuano ya ligi kuu”.
Simba kwa sasa inafanya mazoezi mara mbili,
inaanzia uwanjani na inamalizia ufukweni.
0 comments:
Post a Comment