Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
MSAFARA wa watu 25 wa timu ya Vipers Sc (zamani
Bunamwaya) inayoshiriki ligi kuu nchini Uganda unatarajia kutua leo nchini
tayari kwa mchezo wa kesho wa kimataifa wa kirafiki dhidi ya Wagonga nyundo wa
Mbeya, Mbeya City fc utakaopigwa uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Dar es
salaam.
Msafara huo wenye wachezaji 20 na viongozi 5
utatua uwanja wa Ndege wa kimataifa wa mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es
salaam na kuunganisha Ndege mpaka uwanja wa Ndege wa kimataifa wa Songwe,
jijini Mbeya.
Afisa habari wa Mbeya City, Dismas Ten amesema
maandalizi ya mechi hiyo yamekamilika na kitakuwa kipimo kizuri kwa klabu yao
kabla ya kuanza michuano ya ligi kuu.
Ten aliwataka mashabiki wa klabu hiyo Mkoani Mbeya
na mikoa jirani kujitokeza kwa wingi kuishangilia timu yao.
Kocha mkuu wa klabu hiyo, Juma Mwambusi alisema
kuwa anahitaji mechi ya kimataifa ya kirafiki ili kufanya majumuisho ya
maandalizi yake na kupata kikosi cha kwanza atakachotumia katika kampeni za
kusaka ubingwa.
Mwambusi alisema viongozi walikuwa wanatafuta timu
ya Malawi, lakini ikashindikana na mpaka kufikia jana Vipers ya Uganda
ilithibitisha kuja nchini.
Mwambusi anayesaidiwa na Suleiman Jabir alisema
kuwa wachezaji wake wote wapo katika hali nzuri na wanajiandaa kutoa changamoto
nyingine msimu ujao.
Msimu uliopita, City walishika nafasi ya tatu
nyuma ya Yanga na Azam fc waliotwaa ubingwa.
Mbeya City wataanza ligi kuu kwa kuwakaribisha
maafande wa JKT Ruvu katika uwanja wa Sokoine Mbeya, septemba 20 mwaka huu.
0 comments:
Post a Comment