Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
MAAFANDE wa Tanzania Prisons wametua Dar es salaam
kuendelea na mazoezi ya kujiwinda na mchezo wa ufunguzi wa ligi kuu soka
Tanzania bara utakaopigwa septemba 20 uwanja wa Mabatini mkoani Pwani dhidi ya
wenyeji Ruvu Shooting.
Prisons waliotua juzi Dar wamesema wamewahi kuja
ili kuzoea hali ya hewa ya maeneo ya Pwani ambayo ni joto tofauti na Mbeya
kwenye baridi kali.
Kocha mkuu wa klabu hiyo, David Mwamwaja amesema
wakiwa Dar es salaam wanatarajia kucheza mechi kubwa za kirafiki dhidi ya Azam fc
pamoja na JKT Ruvu ili kujiweka sawa kabla ya kuanza mikikimikiki ya ligi kuu.
“Hali ye hewa ya kwetu ni tofauti na Pwani, kwahiyo tumewahi kuja ili tuzoee na
itatusaidia kufanya vizuri. Tuna mpango wa kucheza na Azam na JKT Ruvu kabla ya
kuanza ligi kuu.” Alisema Mwamwaja.
Kocha huyo aliichukua Prisons mwishoni mwa msimu
uliopita kuinusuru kushuka daraja isingekuwa ushindi wa bao 1-0 katika mechi ya
mwisho dhidi ya Ashanti United, uwanja wa Jamhuri Mkoani Morogoro.
Prisons wasingeshinda mechi hiyo wangeshuka daraja,
wakati Ashanti chini ya Abdallah Kibadeni walikuwa wanahitaji ushindi ili
kuwaacha Wajela jela walikuwa wanalingana nao pointi 25.
Ushindi wa Prisons uliifanya ifikishe pointi 28 na
kuziacha Ashanti, JKT Oljoro na Rhino Rangers zikishuka daraja.
Kuelekea msimu ujao, kocha Mwamwaja alisema
watafanya biashara mapema ili kuepuka mazingira ya kupambana dakika za mwisho.
0 comments:
Post a Comment