Saturday, September 27, 2014


Emmanuel Okwi akishangilia goli lake la kwanza msimu huu  akiichezea Simba sc

Na Baraka Mpenja, Dar es salaam

0712461976

WEKUNDU wa Msimbazi Simba sc wamelazimishwa sare ya 1-1 dhidi ya Polisi Morogoro katika mchezo wa pili wa ligi kuu soka Tanzania bara uliomalizika jioni hii uwanja wa Taifa, Dar es salaam.

Hii ni sare ya pili kwa Simba kwani mchezo wa ufunguzi wikiendi iliyopita waliambulia pointi moja kufuatia sare ya 2-2  na Wagosi wa Kaya, Coastal Union ya Tanga katika uwanja huo huo.

Simba walikuwa wa kwanza kuandika bao la kuongoza kupitia kwa Mganda Emmanuel Anord Okwi katika dakika ya 32, wakati Danny David Mrwanda aliisawazishia Polisi Moro bao hilo katika dakika ya 50 ya kipindi cha pili.

UCHAMBUZI WA MECHI

Kipindi cha kwanza mpira ulianza pole pole, Simba wakitawala zaidi safu ya kiungo chini ya kiungo wa ulinzi aliyerejea baada ya kukaa nje ya uwanja kwa muda mrefu kutokana na majeruhi, Jonas Mkude.

Licha ya kutocheza kwa muda mrefu, Mkude alionesha kiwango kizuri katikati  ya uwanja, alipiga pasi sahihi, alitawala mpira kwa kugusa na kuachia na kuisukuma timu kwenda mbele, huku Piere Kwizera aliyepandishwa juu kidogo akijitahidi kuisaidia timu.

Shaaban Kisiga aliyecheza nyuma ya Tambwe alicheza vizuri, alipiga pasi kama afanyavyo akiwa katika nafasi hiyo, lakini hakuwa katika kiwango chake  kilichozoeleka.

Simba walifika zaidi golini kwa Polisi na mpaka kipindi cha kwanza kinamalizika walipata kona tano kwa tatu. Amissi Tambwe na Emmanuel Okwi walikosa nafasi kadhaa za kufunga.

Dakika ya 26 Okwi alikosa nafasi ya wazi kabisa akidhani ameotoa na mpira ukaokolewa na kipa na kuwa kona ambayo ilizalisha hatari langoni mwa Polisi, lakini Simba wakakosa tena nafasi hiyo.

Okwi alifuta makosa yake na kuandika bao la kuongoza katika dakika ya 32 akimalizia pasi ndefu ya Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ kutoka upande wa  kushoto wa uwanja, huku mabeki wawili wa Polisi akiwemo Lulanga Mapunda wakimuacha Mganda  huyo atulize mpira kifuani katika eneo la hatari na kutikisa nyavu.

Kilichoonekana kubadilika kwa Simba tofauti na mechi iliyopita dhidi ya Coastal Union waliyotoka sare ya 2-2 ni utulivu mkubwa sehemu ya kiungo. Mkude amerejea na mchango wake umeonekana dhahiri.

Lakini mechi hii mpaka dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika, haikufikia hata nusu ya ubora wa mechi iliyopita.

Polisi Moro walianza mechi kwa kulinda zaidi eneo lao na hawakufanikiwa kupiga shoti lolote lililolenga lango.

Waliweka mpango mkakati wa kumkaba Okwi na Tambwe na kila mpira ulipofika walikuwa mabeki watano dhidi ya wachezaji watatu wa Simba.

Haikuwa rahisi kwa Simba kupenya ngoma ya Polisi, lakini baada ya kufungwa bao la kwanza walifunguka na kusogea mbele na wakapata kona moja.

Danny Mrwanda aliyesimama mbele alionekana kupambana, lakini alikuwa na kitu kama ‘jaziba’. Aliingia kwenye mivutano mara kadhaa na mabeki wa Simba.

Mpaka dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika, Simba walikuwa mbele kwa bao 1-0.

Kipindi cha kwanza Polisi walianza vizuri mechi na kudhihirisha kocha wao Adolph Rishard amewaelekeza nini cha kufanya.Walionekana kuwa na nguvu kubwa wakipanda juu na kushambulia.

Katika dakika 50 Danny Mrwanda alifunga goli la kusawazisha baada ya mabeki wawili wa Simba, Masoud Nassor ‘Cholo’ na nahodha Joseph Owino kugongana na kumuacha nyota huyo wa zamani wa Simba akifunga.

Cholo aliteguka mkono na kutolewa kabisa uwanjani na Patrick Phiri akalazimika kumuingiza Willium Lucium ‘Gallas’.

Dakika ya 58 kwenda 59 Ramadhani Singano ‘Messi’ alimmegea pande nzuri Shaaban Kisiga ambaye alimtafuta Tambwe, lakini Mrundi huyo akaukosa na mpira kunyemelewa na Okwi aliyejaribu kupiga, lakini mabeki wakatoa mpira na ikawa kona.

Okwi alichonga kona nzuri kutoka wingi ya kushoto , Tambwe akaruka juu na kupiga kichwa murua, lakini mpira uligonga mtambaa panya.

Mechi iliendelea kuwa na kasi, lakini Simba walikufa katikati na pengine Mkude alipungua kasi kwasababu hajacheza muda mrefu.

Simba wakishika mpira walikuwa wazuri, lakini wakipoteza walikuwa na mipango mibovu na hatimaye kujikuta wakishambuliwa mara kadhaa.

Okwi, Kisiga na Kwizera hawakuweza kurudi nyuma kiufanisi kuisaidia timu inapopoteza mpira, wakati huo huo Mkude akiwa hana kasi ya kutosha nafasi ya kiungo wa ulinzi.

Phiri aliliona hilo haraka na kuamua kumtoa Kisiga na nafasi yake kuchukuliwa na Amri Kiemba ‘Baba wawili’.

Pamoja na kuingia kwa Kiemba, Simba walionekana kutanua sana katikati wakishika mpira, lakini wakipoteza walikuwa wanashindwa kurudi kuzuia mipira kutokea sehemu hiyo muhimu ya timu.

Dakika ya 74 Tambwe alitolewa na nafasi yake kuchukuliwa na Elias Maguli.

Dakika ya 89 uliingizwa mpira wa hatari langoni mwa Simba, Suleiman Kassim ‘Selembe’ alipiga kichwa, mpira ukagonga mwamba na kipa Casillas akaudaka mpira huo.

Dakika za mwisho, Simba walifika langoni mwa Polisi, lakini Amri Kiemba na Singano walishidnwa kutegua mtego wa kuotea.

Kiujumla Simba wameendelea na tabia yao ya kuanza mechi vizuri katika kipindi cha kwanza, lakini kipindi cha pili wanalowa kwa kiasi fulani.

Licha ya kujitahidi kushambulia, lakini Simba walikufa safu ya kiungo nadhani ilitokana na Mkude kuchoka kwa kiwango fulani.

Polisi Morogoro walifunguka na kucheza mpira mkubwa kipindi cha pili. Wangekuwa makini wangefunga magoli kadhaa.


Kocha Phiri analazimika kuwarudisha wachezaji darasani, kuwatafutia kasi ya dakika 90 wachezaji wake na kurekebisha safu ya kiungo.

0 comments:

 
voyeur porn porn movies sex videos hd porno video