Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
LIGI kuu soka Tanzania bara inaendelea leo jioni
kwa mechi tano kupigwa viwanja mbalimbali nchini.
Simba inawakaribisha Maafande wa Polisi Morogoro
katika uwanja wa Taifa, Dar es salaam.
Mechi iliyopita, Simba walitoka sare ya 2-2 na
Coastal Union, wakati Polisi Morogoro walifungwa 3-1 na Azam fc.
Mechi nyingine itakuwa katika uwanja wa Manungu
Complex ambapo Mtibwa Sugar wanaikaribisha Ndanda fc ya Mtwara.
Mtibwa walishinda 2-0 dhidi ya Yanga mechi iliyopita
uwanja wa Jamhuri, Morogoro, nao Ndanda walishinda 4-1 dhidi ya Stand United
uwanja wa Kambarage Shinyinga.
Azam fc watachuana na Ruvu Shooting uwanja wa Azam
Complex, Chamazi, Dar es salaam.
Mabingwa hao watetezi walianza ligi kwa ushindi wa 3-1 dhidi ya Polisi Moro,
wakati Shooting wao walitandikwa 2-0 na Prisons.
Mtanange mwingine utapigwa katika dimba la Sokoine
Mbeya, ambapo Mbeya City fc itachuana na Coastal Union ya Tanga.
Mbeya City wataingia uwanjani wakiwa na kumbukumbu
ya kutoka 0-0 na JKT Ruvu mechi ya ufunguzi, wakati Coastal walitoka 2-2 na
Simba uwanja wa Taifa, Dar es salaam.
Mechi ya mwisho leo hii ni baina ya Mgambo JKT dhidi
ya Stand United ya Shinyanga katika uwanja wa CCM Mkwakwani, Tanga.
Mgambo walishinda bao 1-0 mechi ya ufunguzi dhidi
ya Kagera Sugar uwanja huo wa Mkwakwani, wakati Stand United walitandikwa 4-1
na Ndanda fc kwenye uwanja wao wa Kambarage.
Ligi hiyo itaendelea kesho kwa mechi mbili kupigwa
ambapo Yanga waliotoka kufungwa 2-0 na Mtibwa Sugar uwanja wa Jamhuri watakuwa
nyumbani, Taifa, Dar es salaam kupepetana na Prisons walioshinda 2-0 mechi
iliyopita dhidi ya Ruvu Shooting, Mabatini.
JKT Ruvu waliotoka 0-0 na Mbeya City fc wikiendi
iliyopita Sokoine, watakuwa wenyeji wa Kagera Sugar waliofungwa 1-0 na Mgambo
JKT uwanja wa Mkwakwani Tanga.
0 comments:
Post a Comment