Na Baraka Mpenja, Dar es salam
0712461976
MABINGWA watetezi wa ligi kuu Tanzania bara jioni
ya leo wanawakaribisha maafande wa Ruvu Shooting katika mechi ya raundi ya pili
ya ligi kuu itakayopigwa uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es salaam.
Wakiwa na kumbukumbu ya ushindi wa 3-1 dhidi ya
Polisi Moro wikiendi iliyopita, Azam wanakutana na Ruvu Shooting iliyochapwa
2-0 na Prisons mechi ya ufunguzi (septemba 20 mwaka huu) uwanja wa Mabatini,
Pwani.
Shooting imekuwa ikitoa upinzani mkubwa katika
michuano ya ligi kuu, lakini rekodi ya msimu uliopita inaonesha wazi kuwa
walikuwa dhaifu mbele ya Azam fc, nyumbani na Ugenini (walifungwa mabao 6 bila
majibu kwa mechi zote mbili).
Azam fc kwa asilimia zote walitangaza ubingwa wao
katika mechi dhidi ya Shooting uwanja wa Mabatini wakishinda 3-0.
Leo hii Maafande hawa chini ya kocha Mkenya, Tom
Alex Olaba wanaingia wakiwa na hasira za
kutaka kulipa kisasi, lakini changamoto itakuwa kubwa sana.
Azam fc wameendelea kuwa bora wanapocheza uwanja
wa nyumbani, hata msimu uliopita walikuwa wanatoa dozi kali Azam Complex.
Mazingira ya uwanja huo ni rafiki kwa wachezaji wa
Azam fc. Muda wote wanafanya mazoezi hapo na inapofika siku ya mechi
wanamalizia kazi tu.
Kushinda Chamazi ni ngumu , hivyo Ruvu Shooting wanatakiwa kujipanga barabara.
Kikosi cha kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog
kilianza kwa kupoteza kikombe cha Ngao ya Jamii, septemba 14 mwaka huu kufuatia
kufungwa 3-0 na Yanga.
Didier Kavumbagu (kushoto) atafunga leo tena ?
Katika mechi hiyo, Azam hawakucheza vizuri, walizidiwa ujanja na Yanga, walipoteza mechi kihalali, lakini mechi ya ufunguzi wa ligi kuu dhidi ya Polisi Moro walionekana kuimarika upya na kuwa katika morali ya hali ya juu.
Kinachowabeba wachezaji wa Azam ni mazingira bora ya klabu hiyo. Kwa asilimia kubwa wamekamilika kiuchezaji. Wana utimamu wa mwili, wako sawa kiufundi, kimbinu na kisaikolojia.
Lakini wameendelea kufanya makosa ya uwanjani kama
sehemu ya mchezo. Mpira wa miguu ni mchezo wa makosa.
Makosa yapo, yataendelea kuwepo na ndio kazi ya
makocha kupunguza na kufuta makosa hayo duniani kote.
Katika mechi ya leo Azam wataendelea kuwakosa
washambuliaji wake wawili, Nahodha, John Raphael Bocco ‘Adebayor’ na Mhaiti
Leonel Saint Preux. Hata hivyo, Kipre Tchetche na Didier Kavumbagu wana uwezo
wa kufunga magoli.
Omog anaweza kumuanzisha mchezaji yeyote ambaye
yuko fiti. Azam wana kikosi kikubwa na kila mchezaji anaweza kuonesha kile
alichoagizwa.
Mechi iliyopita, Aishi Manula alianza badala ya
Mwadini Ali. Alicheza vizuri na leo hii Omog anaweza kumpanga tena kama hana
tatizo lolote.
Shomari Salum Kapombe anaweza kucheza beki ya
kulia, kinda Gadiel Michael kushoto au Erasto Nyoni.
David Mwantika na Aggrey Morris wana asilimia zote
kuanza nafasi ya mabeki wa kati. Morris amekuwa katika ubora wake na faida yake
ni kuweza kupanda kuongeza mashambuliaji.
Beki huyo alipanda mara kadhaa kwenye mechi dhidi
ya Polisi na kufanikiwa kufunga goli moja kati ya nafasi kadhaa alizopata.
Morris ni beki wa kisasa. Anaweza kuisaidia timu
kufunga na anaweza kufanya hivyo kutokana na safu bora ya kiungo ya Azam.
Bolou Michael ni kiungo bora wa ulinzi, Salum
Abubakary ‘Sure Boy’ ni kiungo mzuri wa uchezeshaji. Lakini pembeni Himid Mao
na Tchetche wamekuwa na uwezo mzuri wa kuziba mianya ya mashambulizi kutoka kwa
upinzani pale Morris anapopanda juu.
Kama hatachungwa leo, beki huyu wa kati, raia wa
Zanzibar anaweza kufunga tena.
Kutokana na ukubwa wa kikosi cha Azam fc,
kumewafanya wawe na uwezo mkubwa wa kupata matokeo, lakini ligi imebadilika
siku hizi.
Ruvu Shooting ni timu pinzani na msimu uliopita
ilimaliza katika nafasi ya Sita kati ya timu 14. Kikosi chao kimesukwa upya,
kimesheheni vijana wadogo na wakongwe.
Kilizidiwa na Prisons mechi iliyopita na kuifungwa
2-0, lakini ukirejea katika mechi za majaribio ikiwemo waliyofungwa 1-0 na Azam
fc uwanja wa Azam Complex, walicheza vizuri sana.
Leo wanakabiliana na timu bora ikiwa nyumbani
kwake. Ni ngumu sana kupata matokeo, hata historia haiwatendei haki.
Mpira wakati fulani hauheshimu historia, lakini
kuchomoka Chamazi sio jambo jepesi hata kidogo.
Kwa upande wangu, nawapa Azam fc asilimia 80 ya
kuibuka na ushindi, japokuwa mpira una matokeo ya tofauti.
0 comments:
Post a Comment