Monday, September 15, 2014

Na Baraka Mpenja, Dar es salaam

0712461976

MBEYA CITY FC ni klabu inayosubiriwa kwa hamu katika michuano ya ligi kuu kwasababu msimu uliopita ilitoa changamoto kubwa kwa klabu za juu, Simba, Yanga na mabingwa Azam fc.

Katika mechi 26 za ligi kuu,  timu hii inayonolewa na kocha Juma Mwambusi ilifungwa mechi tatu tu ambapo ya Kwanza ilichapwa na Yanga 1-0 uwanja wa taifa.

Mechi ya pili ilipoteza 2-0 dhidi ya Coastal Union Uwanja wa CCM Mkwakwani Tanga na mechi ya tatu ikafungwa 2-1 na Azam fc uwanja wa Sokoine Mbeya.

Ilipocheza na Azam fc uwanja wa Azam Complex, mechi ya mzunguko wa kwanza, City ilitoka sare ya mabao 3-3. Wakati Yanga walilazimisha sare ya 1-1 uwanja wa sokoine mzunguko wa kwanza sawa na Coastal Union ambao walipata matokeo kama hayo katika uwanja huo mgumu kwa timu pinzani.

Mbeya City walifanikiwa kushika nafasi ya tatu nyuma ya Yanga na Azam fc ambao walitwaa ubingwa.

Lakini moja ya matukio ninayoyakumbuka vizuri kwa timu hii ya Mbeya City ni jinsi mashabiki wa Mbeya walivyokuwa na mwamko wa kuishangilia timu yao.

Walisafiri maeneo mengi ambayo City ilikwenda kucheza, hakika walifanya jambo linalotarajiwa kuigwa na watu wa Mtwara kwa Ndanda fc na Shinyanga kwa timu yao ya Stand United.

Wataendeleza?: Mashabiki wa Mbeya City fc waliwahi kupiga mawe gari la Tanzania Prisons

Ukiwafuatilia watu wa Mtwara na Shinyanga, wanatamani sana kufikia mafanikio ya Mbeya City, na wana malengo ya kuzitupa kule timu za Simba na Yanga.

Mashabiki wa Mbeya City wanafaa kuigwa kwa namna wanavyoshangilia timu yao, lakini kuna mambo mawili wanatakiwa kutoigwa kabisa kwasababu hayawezi kuiendeleza timu.

Mosi: kutokukubali  matokeo mabaya, mara nyingi mashabiki wa Mbeya City wanaonekana kuwa na jaziba pale timu yao inapokosea. Wana amini kuwa haki ya kushinda iko upande wao.

Niliwahi kushangaa siku moja ikishida 2-1 dhidi ya Ruvu Shooting. Mashabiki walimzomea kocha Mwambusi wakati matokeo yakiwa sare ya 1-1 mpaka dakika za lala salama kabla ya kufunga bao la ushindi. Kabla ya mechi hiy, City ilitoka sare na Yanga, Kagera Sugar na Coastal Union.

Matokeo hayo yalionekana kuwakera mashabiki wake, licha ya ukweli kuwa yalikuwa mazuri kimpira kwasababu timu ilikuwa ngeni na ilikutana na timu ngumu zenye uzoefu na ligi kuu.

Mashabiki wa Mbeya City fc mara nyingi huwa wanakosa uvumilivu

Kwa watu wa mpira hawakushangaa matokeo kama hayo, kwasababu kuna faida ya kupata pointi moja kuliko kupoteza kabisa. Timu ndio kwanza inaanza, unamzomea mwalimu na wachezaji, kwanini?

Mpira hauko hivyo, hapa mashabiki wa Mbeya City walifeli. Hivyo watu wa Mtwara na Shinyanga, mnatakiwa kuachana na tabia hii kama mnataka kufanikiwa.

Pili; kujihusisha na vurugu. Mara kadhaa mashabiki wa Mbeya City walijihusisha na vitendo vya utovu wa nidhamu kwenye mpira. Waliwahi kurushia mawe basi la Yanga na kupasua vioo hatimaye kumjeruhi dereva uwanja wa Sokoine.

Waliwahi kufanya vurugu kubwa kwenye mechi dhidi ya Tanzania Prisons. Kiufupi wana rekodi ya utovu wa nidhamu na walishaigharimu timu kwa tabia hii. Mara kadhaa City walitozwa faini na TFF.

Hata kwenye mechi ya majaribio ya tiketi za kielekroniki baina ya Mbeya City na Prisons mwaka huu, kulitokea vurugu ambazo hata wachezaji walishiriki, lakini Mwambusi aliwatetea na kudai wanaonewa.

Vurugu hazifai kwenye mchezo, watu wa Mtwara na Shinyanga, hili hampaswi kuiga kabisa.

Lakini jambo jingine ni juzi (jumamosi) walivyofungwa 4-1 na Vipers FC ya Uganda katika mechi ya kimataifa ya kirafiki.

Mashabiki walionekana kukerwa na matokeo na waliowengi walitoka kabla ya mechi kumalizika na leongo likiwa ni kuashiria kutopenda kilichotokea.

Vipers FC ni wazuri kuliko Mbeya City FC na mpira ulionekana uwanjani, lakini mashabiki hawakuwa tayari kukubali kama timu imezidiwa na badala yake wengine wakatoka kabla ya muda.

Yawezekana wengine walikuwa wanawahi usafiri, lakini waliowengi, hususani wa Mbeya mjini walitoka kwasababu ya kukerwa na matokeo.

Haipaswi kuwe hivi katika mpira. Mara ngapi watu wanafungwa, lakini wanashangilia mwanzo mwisho?, hili pia mashabiki wa Mbeya City wamefeli.

Kuna haja ya kubadilika,  watu wa Stand United na Ndanda msijifunze tabia hizi tatu nilizozisema. Mpira hauko hivyo. Na ninyi wa Mbeya City jifunzeni kukubali matokeo, la sivyo mtazidi kupotea katika njia.


Timu yenu ni nzuri, ina kocha mzuri, lakini kama hamtafuta kasumba hii, basi hamtafika mbali kama mnavyodhani.

0 comments:

 
voyeur porn porn movies sex videos hd porno video