Na Baraka Mpenja, Dar es Salaam
KOCHA wa Ruvu Shooting ya Pwani, Mkenya Tom Alex
Olaba amewatema wachezaji sita (6) katika kikosi chake na kuagiza uongozi
utafute nyota wengine kwa ajili ya kukiongezea makali kikosi chake kueleka
msimu mpya wa ligi kuu Tanzania bara.
Afisa habari wa klabu hiyo, Masau Bwire amesema kuwa
uongozi wa klabu hiyo unatarajia kukaa na wachezaji hao sita kuwaeleza ukweli
ili watafute timu nyingine au wakacheze kwa mkopo timu nyingine.
“Olaba ameona hana mpango na wachezaji hao. Lakini
ameainisha sababu za kuwaacha ikiwa ni pamoja na utovu wa nidhamu”.
“Huwezi kuipatia timu mafanikio kama huna nidhamu,
kwahiyo mwalimu ameona bora kuachana nao”.
“Pili ni kushuka kwa kiwango. Kwasasa tuna malengo
makubwa ya kuleta mabadiliko ya soka la Tanzania, lakini kama mchezaji kiwango chake
kimeshuka, sidhani kama anaweza
kuisaidia timu”.
“Kwasababu hiyo, mwalimu Olaba amependekeza waachwe
hata kama wana mikataba au watafutiwe timu wakacheze kwa mkopo”. Alisema Masau.
Aidha, alibainisha kuwa uongozi haujakaa na vijana
hao ili kuzungumza nao, lakini muda wowote mwenyekiti wa klabu Kanali Charles
Nguge atawaita na kuwaeleza ukweli.
Hata hivyo, Masau alisema ni mapema mno kuwataja
majina na akaomba wapenzi wa soka kuwa na subira kwani haraka haraka haina Baraka.
“Kwasababu mwalimu ameshawataja wachezaji hawa,
basi itafika wakati tutawataja ni akina nani, lakini kwasasa tunakamilisha
taratibu”. Aliongeza Masau.
Pia alisema uongozi wa klabu hiyo kwa kushirikiana
na kocha Olaba wameamua kusuka kikosi chao upya kwa kutumia vijana.
“Kuanzia tarehe 15-18 mwezi huu tutakuwa na
majaribio ya kusaka vipaji”.
“Mwenyekiti wa klabu Kanali Nguge ametoa wito kwa
mtanzania yeyote anayejiona ana kipaji cha kucheza mpira kuhudhurie majaribio hayo”. Alisema Masau.
0 comments:
Post a Comment