Na Baraka Mpenja, Dar es Saalam
0712461976
KUFUATIA usajili walioufanya Azam fc kwa wachezaji
wawili wa Yanga SC, kiungo mkabaji, Frank Domayo na mshambuliaji wa kati,
Didier Kavumbagu na kuzua mvutano baina ya wapenzi, wanachama na viongozi wa
klabu hiyo, wachezaji wa zamani wa Yanga wamewataka wanachama kuwa wamoja na
kutoruhusu migogoro kuchukua nafasi.
Domayo na Kavumbagu walisajiliwa mwanzoni mwa wiki
hii ambapo Mrundi ndiye alikuwa wa kwanza kutia sahihi katika fomu za Azam
akifuatiwa na Domayo siku moja baadaye.
Usajili wa Domayo uliwashitua wana Yanga wengi na
kuanza kuhoji iweje uongozi umwachie aende wakati bado wanaona ana msaada
mkubwa kwa klabu.
Domayo alisajiliwa akiwa katika kambi ya timu ya
taifa iliyopo jijini Mbeya kujiandaa na
mchezo wa leo dhidi ya Malawi katika uwanja wa sokoine, lakini si jambo jipya
kwasababu hata Yanga walimsajili miaka miwili iliyopita akiwa kambi ya Stars.
Huu ni usajili uliowagusa wapenzi wengi wa Yanga na
pengine kupandisha hasira kwa viongozi wao.
Kupitia mtandao huu, aliyekuwa makamu mwenyekiti
wa Yanga, bilionea Davis Mosha alilalamika na kuhoji kwanini wachezaji muhimu
waondoke?.
Mosha alienda mbali zaidi na kusema labda kwavile
viongozi wasasa wanaondoka madarakani, hivyo wanataka kuiacha timu haina
wachezaji kwasababu wamesema hawagombei tena.
Mbali na Mosha, wanachama wengine wa Yanga
wamekuwa wakilalamika sana kuondoka kwa nyota wao, hasa kipenzi cha roho zao, kiungo mahiri, Frank Domayo `Chumvi”.
Kutokana na hali hii kuendelea miongoni mwa wana
Yanga, baadhi ya wachezaji wa zamani wa klabu hiyo wamelazimika kupaza sauti
zao na kutoa maoni yao.
Katika mahojiano Maalum, mchezaji mahiri wa zamani
wa Jangwani, Shaban Katwila amesema kwasasa mpira ni ajira , hivyo vijana
wanapomaliza mikataba wana haki ya kutafuta sehemu nyingine yenye masilahi
mazuri zaidi.
Katwila alieleza kuwa kutokana na vijana wengi
kutafuta maisha, viongozi waliopo madarakani wanatakiwa kuwadhibiti wanapoona
wanafaa ili wasiondoke.
“Mpira siku hizi ni ajira. Mchezaji anacheza kwa
ajili ya masilahi, kama wanaelekea kumaliza mikataba, viongozi lazima wachangamkie
kuwaongezea mikataba kama wapo katika mipango”.
“Wakichelewa
kufanya kitu hicho, wachezaji lazima waondoke kwenda kutafuta masilahi
mazuri”. Alisema Katwila.
Aidha, mkongwe huyo wa Yanga aliongeza kuwa
mchezaji anapokuwa na kiwango cha juu anapanda bei na inadidi aongezewe
dau,lakini inaposhindikana hawezi kuacha kutafuta sehemu yenye pesa nzuri.
“Cha msingi ni kufanya maamuzi ya mapema, wakae na
wachezaji na kufanya mazungumzo juu ya mahitaji yao, vinginevyo wataleta ugomvi kwa
wanachama ambao watafirikia kuwa wanapoteza wachezaji kwasababu ya uzembe wa viongozi”.
“Nilisoma sehemu nikasikia walikuwa na mazungumzo
na Kavumnagu, lakini Domayo walishamalizana naye na kilichokuwa kinasubiriwa ni
wakala wake ambaye ni mjomba wake, lakini bado nashangaa kaondoka”.
“Labda kuna vitu aliahidiwa na Azam fc, hii ni
timu yenye pesa”
“ Na kwakuwa wachezaji wetu imewaingia akilini
kuwa mpira ni ajira, asingekataa kuondoka labda kama Yanga wangepanda dau zaidi”.
Alifafanua Katwila.
Nyota huyo wa zamani aliongeza kuwa kwa bahati
nzuri Yanga hawajapoteza sana kwasababu bado wapo katika mashindano ya
kimataifa, hivyo kwa vyovyote vile wachezaji muhimu wanatakiwa kulindwa
kimaslahi, kujengwa kisaikolojia ili waendelee kuwepo mpaka msimu ujao.
“Ushauri wangu; nawaomba viongozi wawe makini sana
kuepuka kujenga mazingira ya kutoaminiwa na wanachama wao. Wafanye maamuzi
sahihi kwa muda muafaka”.
“Wanachama
wasiwe na jaziba, cha msingi wakae na viongozi wao ili suala hili liishe”.
Alimaliza Katwila.
Mbali na Katwila, naye kiungo wa zamani wa Yanga
na Taifa stars, Waziri Mahadhi amesema hadhani kama Domayo na Kavumbagu
wamekosea kwasababu mpira ni biashara.
Mahadhi alifafanua kuwa wachezaji hawa wana
familia zao na maisha yao, hivyo inapotokea sehemu yenye maslahi makubwa,
lazima waende na si dhambi kuondoka kwa soka la kisasa.
“Mpira umebadilika sasa hivi, sidhani kama wanapotokea
watu wenye dau kubwa, mtu mwenye akili timamu hawezi kukataa”.
“Kwa viongozi , nadhani kwa kiasi fulani walifanya
makosa kwasababu kama walikuwa wanawahitaji wasingewaachia kirahisi”.
“Kilichotakiwa ni kungumza nao mapema ili kuwapa
mikataba mipya, lakini kusema viongozi wanaondoka ndio maana wanaachia
wachezaji, mimi sina uhakika, japokuwa walifanya makosa”.
“Angalia mfano Rooney alitaka kwenda Chelsea,
lakini Man United walikuwa wanamhitaji na mkataba unaelekea ukingoni,
yakafanyika maamuzi ya haraka kumuongezea mkataba”.
“Tunaona wenzetu kwa wachezaji muhimu inapobaki
miaka miwili wanaanza kuhangaika kuzungumza nao ili wawabakishe”.
“Lakini unashangaa eti mpaka Domayo anabakiza
mwezi mmoja bado hajasainishwa mkataba
mwingine, hapa viongozi nao wamefanya makosa”. Alisema Mahadhi.
Mahadhi alishauri wana Yanga kuwa watulivu na
kuachana na mivutano kwasababu imeshatokea na wachezaji hawapo tena.
“Wameshateleza,
cha msingi watafute wachezaji wanaofanana au zaidi ya hao ili maisha mengine
yaendelee, lakini kulumbana haisaidie kitu”. Aliongeza Mahadhi.
Kuondoka kwa Domayo na Kuvumbagu kumeonekana ni
pengo kubwa kwa Yanga, lakini jana mshambuliaji wa klabu hiyo, Jeryson John
Tegete aliwashauri wana Yanga kuachana na hilo kwasababu waliobaki wanaweza
kuipataia mafanikio kalbu.
“Tunajua walikuwa muhimu, lakini nashangaa watu
wanawalaumu viongozi.
“Sio ishu kubwa sana, kawaida tu, wapo wengine
watakaoonekana wakipewa nafasi zao.
“ Wasishindwe kulala kisa Domayo na Kavumbagu”.
Alisema Tegete.
Dirisha la usajili bado halijafunguliwa, lakini
Azam fc wameshalipua bomu kwa kugusa mitaa ya Twiga na Jangwani.
0 comments:
Post a Comment