Na Baraka Mpenja, Dar es salaam
BAO pekee la mshambuliaji, John Raphael Bocco `Adebayor` limeipa ushinda taifa Stars
dhidi ya Zimbabwe katika mchezo wa raundi ya awali kabisa kuwania kupangwa hatua
ya makundi ya kushindania tiketi za
kushiriki kombe la mataifa ya Afrika mwakani nchini Morocco.
Bocco alifunga bao hilo katika dakika ya 13 kwa
kumalizia pasi nzuri ya Thomas Ulimwengu.
Katika dakika 45 za kipindi cha kwanza, Taifa
stars walionesha uwezo mzuri, lakini Zimbabwe nao hawakuwa wabaya.
Kukaa nyuma kwa wachezaji wa Zimbabwe kuliwasaidia
kuokoa hatari nyingi langoni mwao.
Tatizo kubwa kwa stars lilikuwa ni viungo wake,
Frank Domayo na Mwinyi Kazimoto kushindwa kupiga pasi za kupenyeza, hivyo
kuwalazimisha John Bocco, Thomas Ulimwengu, Mbwana Samata kugeuka na kuchukua
mipira kwa nyuma na kwenda mbele.
Aina hii ya mpira ilipunguza kasi ya mashambulizi na kuwafanya Zimbabwe
wacheze kwa kujiamini na kuona wanawaweza Taifa stars.
Sehemu ya ulinzi wa kati ya Taifa stars ilikuwa nzuri, lakini beki wa kulia, Shomary
Kapombe hakuwa katika kiwango chake na inawezekana ni kukaa nje ya uwanja kwa
muda mrefu. Naye Oscar Joshua kwa upande wa kushoto alicheza vizuri , lakini
alikuwa mzito kidogo.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi ambapo dakika
ya kwanza tu Taifa stars walikosa bao, nao Zimbabwe wakakosa goli.
Dakika moja baadaye John Bocco `Adebayor ` alikosa
nafasi nyingine baada ya kushindwa kumalizia krosi ya chinichini.
Bado tatizo la Stars lilikuwa kukosa umakini
wanapofika langoni mwa Zimbabwe.
Mbwana Samata na John Bocco kwa nyakati tofauti
walishindwa kuzibadili nafasi muhimu kuwa magoli na kuipa Stars kazi ngumu
katika mchezo wa marudiano mjini Harare nchini Zimbabwe.
Mzani wa mpira katika kipindi hiki cha pili
ulikuwa sawa, lakini Zimbabwe walioneka kuwa na mipango mizuri zaidi.
Hawakujibana katika eneo lao kama kipindi cha
kwanza, walifunguka na kwenda mbele na kuifanya Taifa stars ihangaike.
Kwa soka walilocheza Zimbabwe kipindi cha pili
wameonesha kuwa wanao uwezo wa kubadilika na kucheza kulingana na mazingira.
Ni dhahiri kwa wiki mbili zinazokuja kabla ya
kwenda Zimbabwe, kocha Mart Nooij anatakiwa kufanya maandilizi mazuri zaidi
kwasababu inaonekana mechi itakuwa ngumu.
Zimbabwe hawatakuwa na sababu ya kujibana langoni
mwao, watashambulia kwa muda wote ili kufuta matokeo ya leo.
Moja ya kanuni ya mpira ni kumfunga magoli mengi
mpinzani wako ukiwa nyumbani kwani siku zote ugenini mchezo huwa ni mgumu.
Hata hivyo, Taifa stars wanastahili pongezi kwa
matokeo ya leo kwani kimfaacho mtu chake.
Huwezi kujua nini kitatokea Harare kwasababu hata
Stars wanaweza kushinda pia.
0 comments:
Post a Comment