Na Baraka Mpenja, Dar es Salaam
KIUNGO mshambuliaji wa Mbeya City fc, Deus Kaseke
amefungua milango kwa klabu yoyote inayotaka kumsajili kwa masharti ya kumlipa
maslahi mazuri zaidi.
Kaseke ameueleza mtandao huu kuwa mpira ni kazi
yake na atacheza sehemu atakayopata maslahi makubwa zaidi ya yale anayopata katika klabu yake ya Mbeya
City fc.
“Hakuna anayeridhika na kile anachopata, kila
kukicha unaomba upate zaidi.”
“Ikitokea klabu yenye dau nono kunihitaji,
naondoka zangu”. Kaseke amezungumza na mtandao huu.
“Mtazamo wangu mimi uko hivi, kama ikitokea timu
yoyote itakayonihitaji mimi, nafungua milango na waje wamalizane na klabu yangu”.
“Kama Mbeya City wataridhia niondoke nitafanya
hivyo,kama watakataa sitaweza kulazimisha kwasababu nina mkataba nao, lakini
watatakiwa kuongeza mambo `fulani`”.
Kaseke amekuwa akitajwa kuwa katika mipango ya
kocha wa Simba sc, Mcroatia, Dravko Logarusic na inasemekana katika ripoti yake
aliyokabidhi kwa viongozi kabla ya kwenda kwao kwa mapumziko, ameagiza nyota
huyo asajiliwe.
Akizungumzia tetesi za kuwindwa na wekundu wa
msimbazi Simba sc, Kaseke alisema hakuna mchezaji asiyependa kuchezea klabu
kubwa kama hiyo na wakija na mambo anayoyahitaji atajiunga nayo kwasababu
anatafuta maisha.
“Kama Simba wananihitaji wameona naweza kufiti
katika mfumo wao, kama ikitokeoa nitaenda na kupigana kupata nafasi”. Aliongeza
Kaseke.
Kaseke alisema kwa sasa yuko likizo, lakini
jumatatu ya wiki ijayo anaanza mazoezi binafsi ya kujiweka fiti kabla ya kuanza
msimu mpya wa ligi kuu soka Tanzania bara.
Kuhusu nafasi ya tatu waliyoshika msimu uliopita,
Kaseke alisema walikuwa wageni lakini walijitahidi kwenda sambamba na kasi.
Nyota huyo aliongeza kuwa msimu ujao wataendeleza
pale walipoishia na kutwaa ubingwa au nafasi ya pili ili kuiwakilisha nchi
katika michuano ya kimataifa.
0 comments:
Post a Comment