
Na Baraka Mpenja, Dar ES Salaam
0712461976
KAMA
ilivyokuwa mara ya kwanza kwa Azam fc kutwaa ubingwa wa ligi kuu soka
Tanzania msimu huu wa 2013/2014, ndivyo itakuwa mara ya kwanza kwa klabu
hiyo kushiriki michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika.
Michuano hii ndio mikubwa zaidi barani Afrika kwa ngazi ya klabu, hata timu zinazoshiriki lazima ziwe mabingwa wa nchi zao.
Kwa lugha rahisi ni michuano inayozikutanisha klabu zenye hadhi inayolingana bila kujali ubora za ligi kutofautiana.
Azam fc imekuwa timu ya kwanza nje ya Simba na Yanga kutwaa ubingwa wa Bara tangu mwaka 2000 Mtibwa Sugar ilipofanya hivyo.
Kwa maana hiyo klabu hii inakuwa ya kwanza kushiriki ligi ya mabingwa nje ya Simba na Yanga tangu mwaka 2000.
Hii
ni changamoto nzuri kwa klabu nyingine kutoka nchi tofauti za Afrika
zitakazokuja kucheza hapa nyumbani, kwasababau zinafahamu zaidi uwepo wa
Simba na Yanga.
Ukienda
nchi kama Misri, basi wanajua Tanzania kuna Simba na Yanga tu
kwasababu mara nyingi wanaziona nchini mwao katika mashindano haya.
Rekodi
ya mwaka 2003 waliyoweka Simba kwa kuwavua ubingwa Zamalek ya Misiri
haijatoka akilini mwao na Yanga walivyowahenyesha Al Ahly mwaka huu,
kamwe hawawezi kusahau.
Sasa kama CAF watapanga Azam icheze na klabu yoyote ya Misri, basi Mafarao hawa wataiona klabu mpya kabisa machoni pao.
Bila shaka watakuwa wanajiuliza, Azam wana nini cha ziada mpaka wamezivua ubingwa timu wanazozifahamu za Simba na Yanga?
Hakika itakuwa changamoto kubwa kwa Azam fc mwakani, lakini kila kitu kinawezekana kama mikakati inawekwa.
Azam wamekuwa katika mabadiliko makubwa katika harakati zao za kujiweka klabu bora zaidi Tanzania.
Kumbuka msimu wao wa kwanza wa mwaka 2008/2009 wakiwa chini ya kocha mkuu, Neider dos Santos walimaliza ligi katika nafasi ya 8 .
Malengo yao yalikuwa mbali zaidi na tulishuhudia msimu uliofuata wa 2009/2010 wakibadilisha kocha na kumuajiri Itamar Amorim ambaye aliifanikisha Azam kumaliza katika ya 3.
Baada ya msimu huo kumalizika, Azam fc walituliza akili yao na kuanza kuumiza kichwa kutafuta namna ya kusonga mbele zaidi.
Hatua
ya kwanza ilikuwa ni kusajili wachezaji wazuri na ndipo walianza
harakati zao kwa kumnasa Mrisho Ngassa katika usajili uliovunja rekodi
hapa Tanzania.
Walimnasa Ramadhan Chombo `Redondo`, Jabir Aziz, marehemu Patrick Mutesa Mafisango, na mshambuliaji kutoka nchini Uganda, Peter Ssenyonjo aliyeungana na John Bocco `Adebayor` ambaye msimu huo alikuwa miongoni mwa washambuliaji watatu waliofunga mabao mengi zaidi.
Baada ya kusajili nyota hao, Azam fc wakatupia macho benchi lao la ufundi na kuona kuna haja ya kubadilisha nguvu.
Wakagundua
aliyekuwa Kocha wa timu ya Taifa ya Zanzibar, (Zanzibar Heroes),
Muingereza Sterwart John Hall angekuwa msaada kwao. Walimsainisha
mkataba mwaka 2010 na alikaa mpaka 2012.

Hapo ndipo Azam fc walifanikiwa kucheza michuano ya kimataifa ya kombe la shirikisho kwa mara ya kwanza 2011/2012.
Walionesha
kujipanga kwasababu walifika mpaka raundi ya tatu ambayo walitolewa kwa
shida na wanajeshi wa AS FAR Rabat ya Morroco.
Mechi
ya kwanza walitoka suluhu ya bila kufungana uwanja wa Taifa na
walipoenda Morocco walifungwa mabao 2-1, huku John Bocco akikosa penati
dakika za lala salama ambayo ingewafanya wasonge mbele.
Azam fc walifika raundi hiyo ya tatu baada ya kuzitoa klabu za Al Nasri Juba ya Sudan Kusini na Barrack YC ya Liberia.
Safari ya Azam fc ikaishia hapo, lakini Sterwart alikuwa na ndoto za kuipa ubingwa Azam fc msimu unaofuata.
Baada
ya kuanza msimu wa 2012/2013, Azam walianza vizuri, lakini dosari
ikaingia ambapo kocha mkuu, Sterwart Hall aliondoka fc kwa madai ya
kutoelewana na mabosi wake na kwenda kufanya kazi Kenya, na ndipo Azam
walimwajiri Boris Bunjak kutoka Serbia.
Bunjak hakufua dafu kuiweka Azam katika makali. Uongozi ukampigia magoti Sterwart na kumrudisha msimu huo huo wa 2012/2013.
Sterwart alikomaa na ligi na kufanikiwa kuchukua nafasi ya pili kwa mara nyingine, huku safari hii Yanga wakitwazwa Mabingwa.
Ukiangalia misimu hii miwili, Yanga na Simba walipokezana ubingwa kama kawaida, lakini Azam fc alibaki palepale.
Baada
ya kuanza msimu wa 2013/2014 walifanya vizuri na kutofungwa mechi
yoyote mzunguko wa kwanza, lakini kocha mkuu Sterwart akajiuzulu
mwishoni mwa mzunguko wa kwanza.
Nafasi
yake ikachukuliwa na Mcameroon, Joseph Marius Omog ambaye aliiongoza
Azam kwenye mashindano ya kombe la shirikisho mwaka huu.
Omog alishindwa kuipa mafanikio Azam baada ya kutolewa hatua ya awali kabisa na Feroviario de Beira ya Msumbiji.
Walishinda bao 1-1 Chamazi, na walipoenda msumbiji walifungwa mabao 2-0.
Baada
ya kushindwa katika michuano ya kimataifa, Omog akarudisha akili yake
ligi kuu na kufanikiwa kutwaa ubingwa msimu huu wa 2013/2014.

Ukiangalia
safari nzima ya Azam fc tangu kuanzishwa kwake mwaka 2007, utagundua
kuwa mipango yao mingi inaelekea kufanikiwa japokuwa safari bado ni
ndefu.
Tangu wameanza wanajitahidi kwenda mbele na si kurudi nyuma.
Wakipata hiki wanakuwa na hamu ya kupata kile, ingawa kuna wakati ajali inatokea kama ilivyokuwa kwa kombe la shirikisho.
Safari hii wapo na Omog, kocha mwenye rekodi ya kutwaa kombe la shirikisho mwaka 2012 akiwa na AC Leopard ya Jamhuri ya Congo.
Mcameroon huyo aliifanya Leopard kuwa tishio ambapo aliwapa ubingwa msimu wa 2011/2012 na kuwapa ubingwa wa kombe la shirikisho.
Yalikuwa
mafanikio makubwa kwake, lakini mwaka mwaka 2013 aliondoka zake na
kujiunga na Azam fc akirithi mikoba ya Sterwart Hall aliyejiuzulu.
Kwa kiasi kikubwa, Omog ameikuta Azam fc akiwa imejengwa na Sterwart, na amemalizia vizuri msingi huo na kutwaa ubingwa.
Muingereza aliicha timu haijafungwa, naye Omog akapokea na kuendeleza rekodi hiyo ya kutofungwa katika michuano ya ligi kuu.
Sasa
kinachosubiriwa kwa hamu ni Omog kuiongoza Azam fc kwa mara ya kwanza
katika michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika na si kombe la
shirikisho walilocheza mara mbili.
Mapema
baada ya kutwaa ubingwa, Omog alikiri kuwa mafanikio aliyoyapata
yanatokana na msingi wa kocha Sterwart, hivyo ana deni la kuwafikisha
mbali Azam fc.
Moja ya mikakati yake ni kupata mafanikio katika michuano mikubwa ya kimataifa kama alivyofanya akiwa na AC Leopard.
Lakini alishatoa tahadhari mapema kuwa michuano hiyo ni mikubwa na inazikutanisha klabu kubwa zenye uzoefu.
Si kazi nyepesi kucheza na klabu kama vile Enyimba, Al Ahly, Esperance, TP Mazembe na nyingine nyingi.
Kwa tasfiri yake Omog mwenye uzoefu wa michuano mikubwa barani Afrika, anamaanisha lazima uwe na wachezaji wenye uzoefu mkubwa.
Azam
fc ina wachezaji wazuri na wengi ni vijana, achilia mbali akina Agrey
Moris, Erasto Nyoni, Michael Bolou, Kipre Tchetche, Brian Umony, John
Bocco, Said Morad na wengine waliokaa kwa muda sasa katika soka.
Kuna
nyota wao wachanga kama vile Gadiel Michael, Kelvin Friday, Joseph
Kimwaga, Kipa Mwadini Ally, Aish Manula, Himid Mao, Hamis Mcha `Vialli`
na wengineo.
Asilimia kubwa ya wachezaji wa Azam hawajawahi kukutana na presha ya ligi ya mabingwa zaidi ya kombe la shirikisho.
Michuano wanayokwenda kushiriki inakutanisha timu mabingwa na si makamu bingwa.
Haya
ni mafanikio, lakini lazima wazingatie sana maneno ya kocha wao Omog
kuwa michuano hii inahitaji kuwa na wachezaji wenye uzoefu mkubwa.
Ushauri kwa uongozi wa Azam ni kuwa lazima wazingatie mahitaji ya kocha wao Omog.
Wamwachie kazi ya kutafuta wachezaji anaowataka na wasimwingilie hata kidogo.
Tunaona siasa za Simba na Yanga katika usajili. Inafikia wakati viongozi wanasajili wachezaji bila mwalimu kujua.
Huu
ni usanii mkubwa mno, lakini kwa vile Azam wanaonekana kuwa klabu ya
kisasa, lazima Omog aachiwe kazi ya kutafuta bunduki zenye risasi nyingi
kwa ajili ya ligi ya mabingwa.
Huyu ni kocha mwenye uzoefu na bila shaka anafahamu aina ya wachezaji anaowataka.
Naamini ataongeza nguvu tu kwasababu wachezaji wengi wa Azam wanaokana kuwa katika mipango yake.

Mbali na usajili, ni vyema Azam fc wakaanza maandalizi ya mapema.
Mwakani inaonekana mbali, lakini katika mpira ili ufanikiwe lazima uwe na mchakato.
Kama unatoka pointi A kwenda B, hapa katikati lazima upitie mchakato fulani.
Mchakato
ninaousema ni mambo ya usajili, kuweka timu kambini mapema na kuwaandaa
wachezaji kisaikolojia na kuwaweka pamoja kwa muda mrefu kueleka
mashindano unayokwenda kushiriki.
Lazima
uanze maandalizi ya mbali ili kuimarisha kikosi chako, na hapa Azam
wanatakiwa kujitahidi kuwa na timu isiyotegemea wachezaji fulani.
Kukosekana kwa Tchetche au Bocco kusiathiri chochote katika klabu.
Azam fc bahati nzuri wana kila kitu, fedha zipo, uwanja upo, hosteli zipo, hivyo wanaweza kufanya watakalo.
Kwa
uwekezaji mkubwa walionao katika klabu yao, wanastahili kupata
mafanikio kama TP Mazembe, lakini ili kufikia hapo lazima wawe na
mipango thabiti.
Azam fc jiandaeni mapema na michuano ya ligi ya mabingwa na ligi kuu Tanzania bara msimu ujao.
Hongereni kwa ubingwa wenu, nawatakia mafanikio mema.
0 comments:
Post a Comment