Ofisi
ya Taifa ya Takwimu, Wizara ya Fedha ina jukumu la kukokotoa Pato la
Taifa kwa robo Mwaka ili kuwapatia takwimu kwa wakati, wadau wa takwimu
za Pato la Taifa katika vipindi vifupi vya robo mwaka ili kuweza
kutathmini mabadiliko ya ukuaji wa uchumi.
Ukuaji
halisi wa Pato la Taifa la Tanzania kwa bei za soko uliongezeka kwa
kasi ya asilimia 6.7 katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2013
ikilinganishwa na kasi ya asilimia 6.4 katika kipindi kama hicho mwaka
2012. Jumla ya thamani ya Pato la Taifa katika kipindi husika ilikuwa
Shilingi 5,012,935 milioni mwaka 2013 ikilinganishwa na Shilingi
4,699,884 milioni mwaka 2012.
Ukuaji wa Shughuli za Uchumi za Kilimo na Uvuvi
Shughuli
za kiuchumi za kilimo zilifikia kasi ya ukuaji ya asilimia 5.3 katika
kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2013 zikilinganishwa na asilimia 5.1
ya robo kama hiyo mwaka 2012. Katika kipindi hicho, kulikuwa na mvua za
kutosha katika mikoa inayozalisha mazao kwa wingi. Aidha, maelekezo ya
ma-ofisa Ugani kwa wakulima kama kuchagua aina bora ya mbegu yalisaidia
kuongeza uzalishaji.
Shughuli
za uvuvi zilifikia kasi ya ukuaji wa asilimia 2.4 katika robo ya pili
ya mwaka 2013 ikilinganishwa na asilimia 6.5 katika kipindi kama hicho
mwaka 2012. Kasi ya ukuaji huu ilipugua kutokana na kupungua kwa mavuno ya samaki kutoka kwenye maziwa, mito na mabwawa.
Shughuli za Uchumi za Viwanda na Ujenzi
Shughuli
za uchimbaji madini, mawe na kokoto ziliongezeka kwa kasi ya asilimia
4.3 katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2013 ikilinganishwa na
kuporomoka kwa kasi ya ukuaji wa asilimia 5.1 katika kipindi kama hicho
mwaka 2012. Kuongezeka kwa kasi hii ya ukuaji ilitokana na kuongezeka
kwa uzalishaji wa madini ya almasi na Tanzanite katika robo ya pili ya
mwaka 2013.
Shughuli
za uzalishaji bidhaa viwandani zilifikia kasi ya ukuaji ya asilimia 5.8
katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2013 ikilinganishwa na kasi ya
asilimia 8.2 mwaka 2012. Kupungua kwa kasi ya ukuaji ya asilimia 2.4
(percentage point) kulitokana na kupungua kwa uzalishaji wa sementi,
vyakula vilivyosindikwa na nguo.
Uzalishaji
wa nishati ya umeme ulifikia kasi ya ukuaji wa asilimia 4.5 katika
kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2013 ikilinganishwa na kuporomoka kwa
kasi ya ukuaji ya asilimia 1.1 katika kipindi kama hicho mwaka 2012.
Kuongezeka kwa ukuaji wa nishati ya umeme kwa asilimia 5.6 (percentage
point) kulitokana na kuongezeka kwa uzalishaji wa nishati ya umeme
unaotokana na mafuta na gesi.
Ukuaji wa Shughuli za Uchumi za Utoaji Huduma
Shughuli
za biashara za jumla na reja reja, ukarabati wa magari na pikipiki na
vifaa vingine vya majumbani zilifikia kasi ya ukuaji wa asilimia 5.9
katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2013 ikilinganishwa na kasi ya
asilimia 7.0 katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2012. Kupungua kwa
kasi kwa asilimia 1.1 (percentage point) kulitokana na kupungua kwa
bidhaa zilizotengenezwa hapa nchini na zilizoagizwa kutoka nje ya nchi
zilizouzwa katika kipindi hicho. Shughuli za upangishaji nyumba, na
shughuli zingine za biashara zilifikia kasi ya ukuaji wa asilimia 6.7.
Shughuli
za uchukuzi na mawasiliano zilifikia kasi ya ukuaji wa asilimia 14.8
katika kipindi husika. Shughuli nyingine ni huduma za Hoteli na migahawa
zilizofikia kasi ya ukuaji wa asilimia 3.2; Shughuli za uendeshaji
Serikali zilifikia kasi ya asilimia 5.0, Elimu asilimia 5.7 na huduma za
Afya na shughuli nyinginezo zilifikia kasi ya ukuaji wa asilimia 3.8
katika kipindi hicho.
Imetolewa na:
Morrice Oyuke
Mkurugenzi wa Takwimu za Kiuchumi
Ofisi ya Taifa ya Takwimu
Dar es Salaam
Kwa
mawasiliano zaidi kuhusu Takwimu za Pato la Taifa kwa robo ya pili ya
mwaka 2013, wasiliana na Ofisi ya Taifa ya Takwimu kwenye anuani
zifuatazo:
Mkurugenzi kuu,
Ofisi ya Taifa ya Takwimu,
S.L.P. 796, Dar es Salaam.
Simu: +255 22 212 2722/3/4
Nukushi: +255 22 2130852
Barua pepe: [email protected] Tovuti:www.nbs.go.tz
0 comments:
Post a Comment