![]() |
Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (Nacte) |
Baraza
la Taifa la Elimu ya Ufundi (Nacte), limeendelea kutoa tahadhari kwa
jamii na kuwataka wamiliki wa vyuo binafsi kukamilisha taratibu za
kisheria kabla hatua za kisheria hazijachukuliwa dhidi yao.
Nacte imesema uendeshaji holela
wa sekta hiyo ni sawa na kufanya makosa jinai katika mazingira ya wazi
ambayo mamlaka hiyo haiwezi kufumbia macho.
Katibu
Mtendaji wa Nacte, Dk. Primunus Nkwera, aliyasema hayo alipokuwa
akizunngumza na mwandishi wa habari hizi mjini hapa hivi karibuni.
Dk. Nkwera alisema wamiliki
wote lazima watambue haki na wajibu wa kukamilisha kazi ya usajili wa
vyuo hivyo kabla ya kuanza kwa majukumu yao ikiwa ni pamoja na
ukusanyaji wa fedha kutoka kwa jamii.Alisema bila kufanyika kwa hatua hizo muhimu, vyuo hivyo havitakuwa na uhalali wa kufanya jambo lolote.
Aliongeza kuwa kabla ya kukamilika kwa taarifa ya watafiti na wachunguzi wa masuala ya elimu ambayo Nacte inatarajia kuipata hivi karibuni baada ya kukamilika, imeona vyema kutoa tahadhari kwa wale ambao bado hawajakamilisha taratibu zinazotakiwa.
Dk. Nkwera alisema baada ya muda huo kufikia mwisho, Nacte haitakuwa na muda wa kufanya majadiliano na mtu au taasisi kuhusu nini kifanyike, badala yake itachukua maamuzi ya kuyafunga majengo yote yanayotumika kinyume cha sheria kwa ajili ya kutolea mafunzo hayo.
Aidha, alisema watakaokamatwa kuhusika na makosa hayo, watachukuliwa hatua za kisheria.
Dk. Nkwera, alisema Nacte kwa kutumia mamlaka iliyonayo, itaweka makufuli makubwa katika milango ya majengo hayo kuwazuia watu hao kuendelea na shughuli zozote.
“Tumekuwa
tukitumia diplomasia ya hali ya juu katika suala hili, lakini wahusika
wamekuwa wakipuuza na kudhani Nacte haina mamlaka kamili ya kisheria na
hivyo huendelea kufanya uharibifu kwenye sekta hii kila wakati,”
alisisitiza Dk. Nkwera.
Aidha, Dk. Nkwera, aliwataka
wazazi wanaowapeleka vijana wao katika vyuo hivyo, kuhoji mambo kadhaa
muhimu ikiwa ni pamoja na usajili.
CHANZO: NIPASHE
0 comments:
Post a Comment