WAZIRI
MKUU Mizengo Pinda amesema uwiano wa kibiashara baina ya Tanzania na
China hauko sawa kwa sababu Tanzania inauza nchini China bidhaa ambazo
hazijasindikwa lakini inanunua kutoka huko bidhaa ambazo zimekamilika
(finished products).
Ametoa
kauli hiyo leo mchana (Jumanne, Septemba 10, 2013) wakati akifungua
maonyesho ya bidhaa zinazozalishwa na kampuni za Kichina kwenye ukumbi
wa Diamond Jubilee. Maonyesho hayo yanayotarajiwa kufungwa Ijumaa,
Septemba 13, mwaka huu, yanahudhuriwa makampuni zaidi ya 200 kutoka
majimbo 14 ya China.
“Mazingira
haya ya kibiashara hayaleti usawa wala maendeleo kwa nchi zote mbili,
ni vema wawekezaji wa China wakaangalia uwezekano wa kujenga viwanda vya
kusindika bidhaa hapa nchni ili Tanzania nayo iweze kuuza bidhaa
zilizotoka viwandani badala ya zile ambazo hazijazisindikwa,” alisema.
Alisema
hatua hiyo itaiwezesha Tanzania kuuza bidhaa zilizokamilika siyo tu
hapa nchini, bali kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya
Maendeleo Kusini mwa Afrika na Ukanda Huru wa Kibiashara (Free Trade
Area) ambazo kwa ujumla wake soko lake lina watu zaidi ya milioni 750.
Alisema
kufanyika kwa maonyesho hayo hapa nchini kunasaidia kuonyesha mbinu
mpya za kiteknolojia kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wa Kitanzania.
“Tunahitaji kupata teknolojia za kisasa kutoka kwenu ili tuboreshe
bidhaa zinazozalishwa nchini na ziweze kuuzika China na kwenye masoko ya
kimataifa,” aliongeza.
Akizungumza
na waandishi wa habari mara baada ya kukagua mabanda mbalimbali, Waziri
Mkuu alisema kimsingi maonyesho hayo ni mazuri na yamelenga kufuta
hisia zilizopo kwa watu wengi juu ya ubora hafifu wa bidhaa
zinazozalishwa China.
Hata
hivyo, alisema ameona vitenge vya wax vinavyozalishwa China na kuongeza
kuwa haoni sababu ni kwa nini pamba inayozalishwa nchini isitumike
kutengeneza vitenge kama hivyo endapo watajenga kiwanda chao hapa
nchini.
Mapema,
Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Abdallah Kigoda alisema maonyesho
kama hayo yatasaidia kuongeza biashara siyo tu kati ya Tanzania na China
bali miongoni mwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Wakati huohuo,
Balozi wa China nchini Tanzania, Dk. Lu Youqing alisema China imekuwa
mshirika mkuu wa kibiashara baina yake na nchi za Afrika kwa muda wa
miaka minne mfululizo. Kuhusu uwekezaji hapa nchini, Dk. Lu alisema
mwaka jana China iliwekeza miradi yenye thamani ya dola za marekani
bilioni moja na kati ya Januari na Juni mwaka huu, uwekezaji umefikia
dola za marekani bilioni 2.17.
Alitaja
maeneo makuu ambayo makampuni ya Kichina yanawekeza kuwa ni kwenye
ujenzi wa barabara, umeme, kilimo, viwanda na mawasiliano.
Naye,
Naibu Mkurugenzi wa Biashara za Nje katika Wizara ya Biashara ya China,
Bw. Zhang Xialing alisema Tanzania na China zimekuwa zikishirikiana kwa
muda mrefu katika masuala ya biashara. Alisema kwa mwaka 2012, biashara
baina ya nchi hizo mbili iliongezeka kwa asilimia 50.2 na katika
kipindi cha Januari hadi Juni 2013, biashara imeongezeka kwa asilimia
54.
Alisema
maonyesho hayo yamedhaminiwa Serikali za Majimbo ya Shanghai, Jiangsu,
Zhejiang na Guangdong kwa kushirikiana na Chama cha Wafanyabiashara wa
Tanzania (TCCIA) pamoja na Baraza la Biashara Africa baina ya Tanzania
na China.
0 comments:
Post a Comment