Tuesday, September 24, 2013

Shughuli za uokozi zinaingia siku ya nne tangu jengo la maduka la Westgate jijini Nairobi kushambuliwa na magaidi Jumamosi na kusababisha zaidi ya watu 60 kuuwawa na wengine wengi kupata Majeraha.
Jeshi la Kenya  
Serikali ya Kenya kupitia Waziri wa masuala ya ndani Joseph Ole lenku imesema imelidhibiti jengo zima na kuwauwa baadhi ya wanachama wa kundi la Al Shabaab waliokiri kutekeleza shambulizi hilo, lakini hii leo asubuhi milio ya risasi ilisikika ndani ya jengo hilo, hali inayoashiria wazi kuwa bado magaidi wapo ndani ya jumba la Westgate.
Hata hivyo Waziri huyo amesema kwamba wamefanikiwa kuwauwa angalau wapiganaji wawili wa kundi hilo la Al Shabaab lililo na mafungamano na kundi la kigaidi la Al Qaeda.
Jengo la biashara la Westgate 
Magaidi hao walifika katika jengo hilo na kuanza kuwamiminia risasi raia waliokuwa katika jengo hilo la biashara.
Kulingana na waandishi habari waliopiga kambi kilomita 70 nje ya jengo hilo wanasema magari ya wazima moto, magari ya kusafirishia wagonjwa na hata wafanyakazi wa Shirika la msalaba mwekundu walikusanyika katika eneo hilo tayari kutoa usaidizi wao kwa majeruhi au matekwa wanaoaminika bado wapo ndani ya jengo.
Wakati huo huo wakenya wamekuwa wakitiana moyo na kuhimiza uwepo wa amani nchini na kuungana pamoja wakati huu ambapo taifa linaomboleza kutokana na shambulizi hilo la kigaidi lililowajeruhi zaidi ya watu 200.
Al Shabaab wazungumzia shambulizi
Huku hayo yakiarifiwa wapiganaji wa kundi la kigaidi la Al Shabaab limesema kwamba bado wanawashikilia watu kadhaa mateka ndani ya jengo hilo. Kundi hilo la kigaidi limesema bado linashikilia msimamo wao.
Awali walisema kwamba iwapo Kenya inataka kuwa na amani katika taifa hilo basi ni lazima waondowe jeshi lake nchini Somalia lililotumwa huku kupambana dhidi ya magaidi hao.
Kutokana na ujumbe wao waliouwasilisha katika mtandao wa kijamii wa Twitter kundi hilo limesema kwamba mateka wanaowashikilia wote wako hai.
Hata hivyo maafisa wa usalama wanasema kwamba wamefanikiwa kuwaokoa mateka kadhaa japo kwa sasa hawana idadi kamili ya wale waliobakia ndani ya jengo nawapiganaji hao wa Al shabaab.
Fatou Bensouda alaani shambulizi la Westgate
Kwa upande wake mwendesha mashtaka mkuu wa mahakama ya uhalifu wa kivita ICC ilioko The hague Uholanzi Fatou Bensouda amesema amelaani kitendo hicho cha kigaidi na kusema kuwa ICC iko tayari kusaidia kuwafungulia mashtaka wale walioshirikiana na magaidi kupanga shambulio la Westgate.
Mwendesha mashtaka ICC Fatou Bensouda  
Bensouda ametoa pole zake kwa waathiriwa .Jumatatu mahakama hiyo ya ICC ilimruhusu makamu wa rais nchini Kenya William Ruto kurudi nyumbani kwa muda wa wiki moja ili kuwa na wakenya katika wakati huu wa shambulizi.
Ruto na mshitakiwa mwenzake mwandishi habari Joshua Arap Sang wanakabiliwa na makosa ya uhalifu dhidi ya ubinaadamu wanayodaiwa kufanya katika ghasia za baada ya uchaguzi mwaka 2007.
Katika hotuba yake makamu wa rais william Ruto alisema kwamba serikali itafanya kila liwezalo kuhakikisha kuwa kenya ni salama kwa wawekezaji, watalii, na kila mkenya na kuwa nchi hiyo haitayumbishwa na mashambulizi ya kundi la Al Shabaab linalojaribu kuwagawanya wakenya kwa misingi ya kidini.
Mwandishi: Amina Abubakar/AP/AFP/ The Standard/ Daily Nation
Mhariri: Mohammed Abdul Rahman
CHANZO: IDHAA YA KISHWAHILI YA DW

0 comments:

 
voyeur porn porn movies sex videos hd porno video